KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 6, 2010

Wamarekani wampania Rooney


LOS ANGELES, Marekani
BEKI wa zamani wa kimataifa wa Marekani, Alexi Lalas amewataka wachezaji wa timu hiyo kuhakikisha wanammaliza mapema mshambuliaji Wayne Rooney wa England katika mechi ya ufunguzi ya Kombe la Dunia kati yao, itakayochezwa Juni 12 mwaka huu.
Alexi alisema juzi mjini hapa kuwa, wanapaswa kuhakikisha Rooney anaonyeshwa kadi nyekundu katika mechi hiyo ili kufifisha matumaini ya England katika fainali hizo.
Beki huyo wa zamani wa Marekani alisema, anaamini hasira za Rooney zinaweza kuigharimu England katika fainali hizo.
“Hakuna ubaya kutumia udhaifu wa mchezaji kumsababishia matatizo uwanjani,”alisema mkongwe huyo, aliyekuwemo kwenye kikosi cha Marekani kilichoifunga England mwaka 1993.
“Ni mwepesi wa kupandwa na hasira, ningependa kumuona akifanya vitendo uwanjani kama mtoto mdogo,”alisema.
Alexi aliiponda England kwa kujiona kuwa ni timu bora kuliko zingine zilizopangwa kwenye kundi C.
“Nafikiri wanayo timu nzuri, lakini inawezekana si timu nzuri kama wanavyofikiria wao,”alisema.
Wakati huo huo, mshambuliaji nyota wa Argentina, Lionel Messi amekiri kuwa, Wayne Rooney ndiye tegemeo kubwa la England katika fainali za Kombe la Dunia.
Messi alilieleza gazeti la The Sun juzi kuwa, kwa kushirikiana na Steven Gerrard na Frank Lampard, Rooney anaweza kuiongoza England kufanya maajabu katika fainali hizo.
“Nafikiri Rooney ni mchezaji mzuri, si tu kwa yale aliyoyafanya mwaka huu,”alisema.
“Kwa miaka mingi sasa, amekuwa akionyesha kwamba ni mmoja wa wachezaji nyota wa kizazi chake na kadri miaka inavyosonga mbele, kiwango chake kimekuwa kikizidi kupanda,”aliongeza.
Messi alisema Rooney ni mchezaji aliyekamilika, ana uwezo mkubwa wa kukaa na mpira miguuni, ana nguvu na uwezo wa kufunga mabao.

No comments:

Post a Comment