KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, September 4, 2013

TUNATAFUTA NAFASI YA PILI-KIM



KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Kim Poulsen amesema wanaipa umuhimu mkubwa mechi yao ya mwisho ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia kwa lengo ni kuhakikisha wanamaliza wakiwa wa pili katika kundi lao.

Taifa Stars iliondoka nchini jana kwa ndege ya Kenya Airways kwenda Banjui, Gambia kwa kupitia Dakar, Senegal huku ikiwakosa nyota wake sita kutokana na kuwa majeruhi na wengine kushindwa kuripoti kambini.

Pambano kati ya Taifa Stars na Gambia linatarajiwa kuchezwa mwishoni mwa wiki hii na litakuwa la kukamilisha ratiba kwa vile timu zote mbili hazina matumaini ya kusonga mbele.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam juzi, Kim alisema wanataka kushinda ugenini, kwani licha ya kuwa wameshatolewa, ushindi utawaongezea pointi kwa ajili ya viwango (rankings) vya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Kim alisema ushindi katika mechi hiyo pia utaiwezesha Taifa Stars kuepuka kuanzia ngazi ya awali ya mechi za mchujo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa fainali za 2015.

 “Tunacheza mechi hii tukiwa katika mazingira magumu, kwani wengi wa wachezaji wa kikosi cha kwanza ni majeruhi. Sijawahi kukutana na hali hii tangu nilipoanza kuifundisha Taifa Stars, lakini tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri,” alisema Kim.

Kim alisema kwa mipango ya timu yake, mechi hiyo ni muhimu tofauti na wengi wanavyofikiria na uamuzi wake wa kumwita beki Henry Joseph, umezingatia mambo mengi ya kiufundi, ikiwemo nafasi anayocheza na uzoefu alioupata katika  klabu yake ya Kongsvinger IL ya Norway.

Wachezaji majeruhi katika kikosi hicho ni Shomari Kapombe, Kelvin Yondani, Aggrey Morris, Salum Abubakar, Athuman Idd na John Bocco.

Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu hawatakuwemo kwenye safari hiyo baada ya klabu yao ya TP Mazembe kutuma taarifa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) jana ikidai ni wagonjwa.

Wachezaji walioondoka jana kwenda Gambia ni Juma Kaseja, Mwadini Ali, Ali Mustafa, Amri Kiemba, David Luhende, David Mwantika, Erasto Nyoni, Frank Domayo, Haruna Chanongo, Henry Joseph, Jonas Mkude, Juma Liuzio, Khamis Mcha, Mrisho Ngasa, Nadir Haroub, Said Dilunga, Simon Msuva na Vincent Barnabas.

No comments:

Post a Comment