KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, September 14, 2013

TENGA AIPONGEZA KAMATI YA LIGI KUU




Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ameishukuru Kamati ya Ligi kwa usimamizi mzuri tangu ilipokabidhi Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) katika mzunguko wa pili msimu uliopita.

Amesema TFF iliamua kuanzisha Kamati ya Ligi kwa lengo la kutaka klabu zijisimamie zenyewe ili kuongeza ufanisi, jambo ambalo limeleta mabadiliko kwa vile hivi sasa hakuna matatizo katika kuwalipa marefa na makamisha wanaosimamia VPL na Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

“Fedha za udhamini sasa zinakwenda moja kwa moja kwenye Kamati ya Ligi. Ni matarajio yangu kuwa ufanisi utaongezeka, kwani tumeanzisha jambo hili kwa lengo la kuleta tija, maendeleo na utulivu,” amesema Rais Tenga wakati akizungumza na Wahariri wa Michezo kutoka vyombo mbalimbali vya habari.

Rais Tenga amesema mahali penye utulivu na utawala bora watu wanakuwa na imani hasa katika masuala ya fedha, hivyo ni lazima kwa kampuni kuwekeza kwa vile kunakuwa hakuna vurugu.

Amesema ukiondoa Afrika Kusini na Angola katika ukanda huu wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini, Ligi Kuu ya Tanzania ndiyo yenye udhamini mkubwa kupitia mdhamini wa ligi na udhamini wa matangazo ya televisheni.

Pia amesema kuanzia msimu ujao 2014/2015 klabu za Ligi Kuu hazitaruhusiwa kusajili wachezaji hadi zitakapowasilisha TFF ripoti zao za mapato na matumizi zilizokaguliwa (Audited accounts), hivyo klabu husika zijiandae kwa ripoti hizo za Januari hadi Desemba 2013.
Kuhusu tiketi za elektroniki, Rais Tenga amesema bado linafanyiwa kazi na CRDB ambayo ndiyo iliyoshinda tenda hiyo na liko katika hatua nzuri, kwani nia ya TFF na benki hiyo kuona kuwa linaanza haraka iwezekanavyo.

“Tiketi za elektroniki zimechelewa kuanza kwa sababu ambazo haziwezi kuzuilika, lakini CRDB imeshatengeneza miundombinu katika karibu viwanja vyote. Kulitokea uchelewaji katika kuleta printer (mashine za kuchapia), zilizokuja hazikuwa zenyewe. Kwa upande wa Uwanja wa Taifa, system (mfumo) iliyopo inatofautiana na ile ya CRDB. Hivyo sasa tunaangalia uwezekano wa zote mbili zitumike kwa pamoja, kwa sababu Uwanja wa Taifa una system yake tayari. Printer zimeshafika, tunataka ili suala lisitucheleweshe,” amesema.

WACHEZAJI 620 WATHIBITISHIWA USAJILI FDL
Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imethibitisha usajili wa wachezaji 620 kati ya 624 wa timu za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inayoanza kutimua vumbi kesho (Septemba 14 mwaka huu).

Wachezaji wanne ambao usajili wao umezuiwa mpaka watakapokamilisha taratibu ni Emmanuel Simwanza Namwando wa African Lyon, Godfrey Bonny Namumana (Lipuli FC), na Enyinna Darlington na Chika Keneth Chukwu wote wa Mwadui FC ya Shinyanga.

Darlington na Chukwu ambao wote ni Wanigeria wamezuiwa mpaka watakapowasilisha vibali vya kufanya kazi nchini kutoka Idara ya Uhamiaji wakati Namumana aliyekuwa akicheza nchini Nepal bado hajapata Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC).

Nayo African Lyon imetakiwa kufikia muafaka na AYOSA Academy ambayo Namwando anatoka juu ya usajili kabla ya kuanza kumtumia mchezaji huyo.

Klabu ambazo zimemaliza nafasi zote 30 usajili katika FDL ni Friends Rangers FC ya Dar es Salaam, na Stand United FC ya Shinyanga wakati iliyosajili wachezaji wachache zaidi ni Burkina Faso FC. Klabu hiyo ya Morogoro imesajili wachezaji 19 tu.

Vilevile Kamati hiyo vilevile imethibitisha usajili wa wachezaji wanane wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) waliosajiliwa katika hatua ya pili ya usajili iliyoanza Agosti 14 hadi 30 mwaka huu.

Wachezaji hao ni Samir Ruhava na Amani Simba (Ashanti United), Robert Machucha na Said Ndutu (Yanga U20), Ayoub Masoud na Abdallah Selemani (Coastal Union U20), Ramadhan Kipalamoto (Simba U20) na Henry Joseph (Simba) ambaye tayari Hati yake Uhamisho wa Kimataifa (ITC) imeshawasili.

No comments:

Post a Comment