KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 26, 2011

WACHEZA FILAMU WA KIKE WANAONG'ARA BONGO

KWA kipindi kirefu sasa, fani ya filamu imekuwa ikijipatia umaarufu mkubwa hapa nchini, ikiwa ni pamoja na baadhi ya wasanii wake kujizolea sifa lukuki na pesa nyingi kutokana na umahiri wao katika uigizaji. Wafuatao ni waigizaji 10 wa kike wa filamu, ambao wamejizolea sifa na umaarufu mkubwa hapa nchini.

ZAMDA SALIM
Ni mshiriki mpya katika fani ya uigizaji filamu, lakini umakini na mvuto wake ni miongoni mwa mambo yaliyomwezesha kupata sifa na umaarufu mkubwa. Ameshiriki kucheza filamu nyingi na ambazo zilitingisha anga la Bongo kama vile Unfortunate Love, Born Again, Hot Friday na Pigo, ambayo aliicheza vizuri zaidi.

WEMA SEPETU

Alikuwa mrembo wa Tanzania mwaka 2006. Aliingizwa kwenye fani ya uigizaji filamu na mpenzi wake wa zamani, Steven Kanumba. Licha ya kukumbwa na kashfa nyingi, ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani mara kwa mara, Wema ni mmoja wa waigizaji nyota na wenye mvuto nchini. Baadhi ya filamu alizoshiriki kuzicheza na kujipatia sifa ni pamoja na A Point of no Return, Fake Pastor, White Maria na My Diary, ambayo ameicheza kwa kushirikiana na Jackline Wolper na Rose Ndauka kupitia kampuni yao ya Jerowe.




WASTARA JUMA

Mwanadada huyu ni mmoja wa wacheza filamu wanaochupikia hapa Bongo, akiwa maarufu zaidi kwa jina la Stara. Mbali na kucheza filamu, fani nyingine ya Stara ni uandishi wa habari. Alianza kujijengea jina alipocheza filamu ya 2 Brothers na baadaye Mboni Yangu. Filamu zingine, ambazo hata yeye mwenyewe anazikubali ni Vita Mkomanae na Vivian.



RIYAMA ALLY

Jina lake si geni katika fani ya filamu hapa nchini. Alianza kuonyesha makali yake katika tamthilia ya Fungu la Kukosa, iliyokuwa ikirushwa hewani na kituo cha televisheni cha ITV. Ameshiriki kucheza filamu nyingi, lakini zilizompatia sifa na umaarufu ni kama vile Mwasu, Alfa na Omega na Second Wife. Ni mwanadada mwenye sura na umbo lenye mvuto.



NDUMBAGWE MISAYO

Anajulikana zaidi kwa jina la Thea. Ni msanii, ambaye kwa sasa huwezi kuacha kumzungumzia ama kumkosa katika fani ya filamu. Alianza kujulikana akiwa katika kundi la Sanaa la Kaole. Ameshiriki kucheza filamu nyingi kama vile Segito na Suspense. Moja ya sifa zake ni mvuto na kuuvaa uhusika wa nafasi anazocheza kiusahihi.



YVONNE CHERRLY

Ni maarufu zaidi kwa jina la Monalisa. Ni mmoja wa wacheza filamu wakongwe hapa nchini, akiwa ameanzia katika kundi la Mambo Hayo, lililokuwa likionyesha tamthili zake kupitia kituo cha televisheni cha ITV. Amewahi kushiriki kwenye filamu nyingi kama vile behind the Scene, Binti Nusa. Filamu yake ya kwanza ni Girlfriend. Kwa sasa ni mtunzi na mtayarishaji wa filamu.




JACKLINE WOLPER

Ni mwanadada mwenye sura yenye mvuto. Ni msanii wa kike aliyeshiriki kucheza filamu nyingi, lakini zilizomwezesha kumjengea sifa na umaarufu ni Surprise na Secretary. Pia ameshiriki kuandaa filamu mpya ya My Diary akishirikiana na Rose Ndauka na Wema Sepetu.


IRENE UWOYA

Kama ni sura tu na umbo, mwanadada huyu, ambaye ni mke wa mwanasoka mmoja maarufu wa Burundi anatisha. Ni mwigizaji aliyedhihirisha kwa vitendo kwamba hapendi mchezo. Baadhi ya filamu alizoshiriki kucheza na kujipatia umaarufu ni pamoja na Mid Night na My Dreams. Irene, ambaye naye hana jina la utani, pia amewahi kutayarisha filamu ya Oprah on Sunday, ambayo imezidi kumng’arisha.




ELIZABETH MICHAEL

Ni maarufu zaidi kwa jina la Lulu. Ni binti anayejaribu kwa kasi kubwa kutishia nafasi za wakongwe katika fani hiyo. Alianza kujihusisha na uigizaji katika kundi la sanaa la Kaole kabla ya kujitosa rasmi kwenye fani ya filamu. Ameweza kufanya vizuri katika filamu nyingi kama vile Family Tears na Reason to die. Ni binti mwenye sura na umbo lenye mvuto.




AUNTY EZEKIEL

Ni mmoja wa wacheza filamu nyota wa kike hapa nchini, akiwa ameshiriki kucheza filamu nyingi na zilizotingisha anga la Bongo kama vile Young Billionaire, Mask na Hard Love Moro, ambayo aliitayarisha. Pia ni mmoja wa wamiliki wa Kampuni ya Filamu ya Jawero, akishirikiana na Rose Ndauka na Jackline Wolper. Kwa pamoja wametoa filamu mpya inayoitwa My Diary.




ROSE NDAUKA

Msanii huyu ameshiriki kucheza filamu nyingi. Filamu ya kwanza kumtambulisha katika ulimwengu huo hapa nchini ni Swahiba. Mbali ya kucheza filamu, Rose ambaye hana jina la utani, kwa sasa ni mtunzi na mtayarishaji wa fani hiyo. Pia ni mmoja wa wamiliki wa Kampuni ya Filamu ya Jawero, akishirikiana na Jackline Wolper na Wema Sepetu. Hivi karibuni walishirikiana kuandaa filamu ya My Diary.

No comments:

Post a Comment