KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 22, 2014

KILI MARATHONI MAMBO YAIVA, VIINGILIO VYATAJWA


Na Ibrahim Kyaruzi, Dar es Salaam
MAANDALIZI ya mbio za 12 za Kilimanjaro Marathon zinazotarajiwa kufanyika Machi 2, 2014 huko Moshi yanaendelea kushika kasi baada ya waandaaji wa mbio hizo kutangaza ada za ushiriki pamoja na ratiba ya mbio hizo.

John Addison, Mkurugenzi Mkuu wa Wild Frontiers, waandaaji wa mbio hizo alisema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana kwamba mbio ndefu za 42km Kilimanjaro Premium Lager Marathon zitaanza saa 12:30 asubuhi huku mbio za 10km Gapco Disabled Marathon zikianza saa 12:45 asubuhi, Nusu Marathon km 21 saa 1 kamili asubuhi na mbio za kujifurahisha za Vodacom 5km Fun Run zitaanza saa moja na robo asubuhi. 
Alisema ratiba hii imepangwa kwa mtiririko huu ili kuwapa fursa washiriki wa kila mbio kuona mandhari ya mji wa Moshi na Mlima Kilimanjaro.
Alisema kuwa viingilio vya mbio ndefu za Full Marathon km 42 viingilio itakuwa ni dola 60 kwa washiriki wa kimataifa, Tsh 6,000 kwa raia wa Afrika Mashariki na dola 30 kwa raia wa kigeni wanaoishi au kufanya kazi Afrika Mashariki wakati huku Nusu Marathon viingilio ikiwa ni dola 60 kwa washiriki wa kimataifa, shilingi 4,000 kwa raia wa Afrika Mashariki na dola 30 raia wa kigeni wanaoishi Afrika Mashariki
Aidha, washiriki wa kimataifa kwenye mbio za walemavu za GAPCO watalipia dola 10, shilingi 3,000 kwa raia wa Afrika Mashariki na dola tano kwa raia wa kigeni wanaoishi Afrika Mashariki.

Mbio hizo za walemavu zitahusisha shindano la mbio za kutumia baiskeli za mikono (Handcycle) na viti vyenye magurudumu (Wheelchair) tu. Washiriki wa kimataifa na raia wa kigeni waishio Afrika Mashariki watalipa dola mbili na raia wa Afrika Mashariki watalipa shilingi 3,000 mbio za kujifurahisha za Vodacom 5km Fun Run.
Kwa mujibu wa Addison, umri wa kushiriki mbio za kilomita 42 ni miaka 21, miaka 18 kwa nusu marathon na mbio za walemavu huku kwenye mbio za kujifurahisha ikiwa ni miaka kumi. "Tutasajili washiriki kwa muda wa siku mbili kabla ya mbio ambapo kwenye hoteli ya Keys Hotel mjini Moshi tarehe 28 Februari na tarehe 1 Machi kuanzia saa 4 asubuhi mpaka saa 11 jioni kila siku na pia uandikishwaji utafanyika Arusha tarehe 27 Februari katika eneo ambalo litatangazwa badae," alisema.
Mbio hizo zinadhaniwa kuwa kati ya mbio kubwa zaidi duniani za kitalii na ndio tukio kubwa zaidi la kimichezo Tanzania. Kilimanjaro Marathon ya mwaka huu inatarajiwa kuwa na washiriki zaidi ya 6,000 wakiwemo takribani wageni 600 kutoka nchi zaidi ya 40.
Kilimanjaro Marathon 2014 inadhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager (wadhamini wakuu), Vodacom Tanzania (5km Fun Run), GAPCO (10km Disabled Run), FNB Tanzania, TPC Sugar, Simba Cement, KK Security, Kilimanjaro Water, Keys Hotel, TanzaniteOne na UNFPA.

No comments:

Post a Comment