KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, September 15, 2011

Clarion aweka kando uigizaji filamu



LAGOS, Nigeria
BAADA ya ukimya wa muda mrefu, mcheza filamu nyota wa Nollywood, Clarion Chukwurah amesema ameamua kujiweka kando na fani hiyo ili apate muda wa kutosha wa kushughulikia taasisi yake binafsi.
Clarion alisema wiki hii kuwa, amekuwa akipata ofa nyingi za kucheza filamu mpya kwa malipo makubwa, lakini kwa sasa ameamua kutumia muda wake mwingi kushughulikia taasisi hiyo, inayojulikana kwa jina la Clarion Initiative.
Mwanamama huyo mwenye mtoto mmoja, wiki iliyopita alisherehekea kutimiza miaka 32 tangu alipojitosa kwenye fani hiyo na kujizolea sifa lukuki.
Kwa mujibu wa Clarion, taasisi yake hiyo inajihusisha na masuala ya kutoa elimu ya uongozi kwa vijana waliopo kwenye shule za sekondari nchini Nigeria kuhusu mambo mbalimbali.
“Tunataka kuwaandaa vijana ili waweze kujiajiri baada ya kumaliza masomo yao badala ya kusubiri ajira za serikali,” alisema na kuongeza kuwa, taasisi hiyo inafanyakazi kwa karibu na USAID, British Council na Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa.
Clarion alisema taasisi yake hiyo ilianza kufanyakazi tangu mwaka 1999 na inajulikana katika nchi za Cameroon, Uingereza, Canada na zinginezo duniani.
Hata hivyo, Clarion hakuwa tayari kuzungumza lolote kuhusu mumewe, ambaye wametengana. Alisema masuala yafamilia yake yanawahusu wao binafsi.
Mcheza filamu huyo alisema ni vigumu kuwalinganisha waigizaji wa Nigeria na nchi kama Marekani kimalipo kwa sababu hata bajeti za kuandaa filamu katika nchi hizo zinatofautiana.
Alisema hafikirii kwenda kuishi nje ya Nigeria kwa sababu moja ya malengo yake ni kujiendeleza zaidi kimaisha na pia kuvisaidia vizazi vijavyo katika mambo mbalimbali.

No comments:

Post a Comment