KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, September 23, 2011

VIINGILIO SIMBA NA MTIBWA

Mechi namba 50 ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Mtibwa Sugar itachezwa Jumapili (Septemba 25 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa ifuatavyo; viti vya kijani na bluu sh. 5,000, viti vya rangi ya chungwa sh. 7,000, VIP B na C sh. 15,000 wakati VIP A itakuwa sh. 20,000.

Mauzo ya tiketi yatafanyika siku ya mchezo kwenye magari mbalimbali yatakayokuwa yameegeshwa nje ya Uwanja wa Taifa.

Uwanja wa Taifa pia utakuwa mwenyeji wa mechi nyingine ya ligi hiyo kati ya Yanga na Coastal Union. Mechi hiyo itachezwa Jumatano (Septemba 28 mwaka huu).

MBWA WA POLISI CCM KIRUMBA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko tukio la mbwa wa polisi kukata kamba na kusababisha mtafaruku kwa wachezaji wakati wa mechi kati ya Toto Africans na Simba iliyochezwa Septemba 21 mwaka huu Uwanja wa CCM Kirumba.

Tunafanya mawasiliano na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza ili kujua chanzo cha tukio hilo, na hatua ambazo jeshi hilo limechukua kwa mhusika iwapo itathibitika kuwa kitendo hicho kilisababishwa na uzembe. Pia tunaamini kuwa tukio hilo litakuwa ni fundisho kwa askari polisi ambao badala ya kufanya shughuli iliyowapeleka uwanjani ya kulinda usalama ugeuka kuwa watazamaji wa mpira.

MAPATO TOTO AFRICANS v SIMBA

Pambano namba 44 la Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Toto Africans na Simba lililochezwa Septemba 21 mwaka huu Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza limeingiza sh. 24,044,000. Viingilio katika mechi hiyo iliyomalizika kwa sare ya mabao 3-3 vilikuwa sh. 2,000 kwa mzunguko na sh. 10,000 kwa jukwaa kuu.

LIGI DARAJA LA KWANZA

Timu saba kati ya 18 za Ligi Daraja la Kwanza bado hazijawasilisha usajili wao wakati ligi hiyo inatarajia kuanza mapema mwezi ujao. Timu hizo ni Temeke United, 94 KJ, Polisi Morogoro, Samaria FC, Rhino FC ya Tabora, Morani FC ya Manyara na AFC ya Arusha.

Ingawa timu kumi na moja zimewasilisha usajili wao, lakini ni sita tu ambazo zimelipa ada ya ushiriki ya sh. 200,000. Timu zilizolipa ni Polisi Iringa, Burkina Faso ya Morogoro, Mlale JKT ya Ruvuma, Morani FC ya Manyara, Mgambo Shooting, Samaria FC na Transit Camp. Timu nyingine za Daraja la Kwanza ni Polisi Dar es Salaam, Tanzania Prisons, Mbeya City Council, Polisi Tabora, Small Kids ya Rukwa na Majimaji.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment