KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, October 23, 2016

MANJI: AHADI YA UWANJA KAUNDA IKO PALEPALE


MWENYEKITI wa Yanga, Yussuf Manji amesema kwamba bado ana matumaini ya kuijengea klabu Uwanja wa kisasa eneo la Jangwani, Dar ea Salaam.
Aidha, Manji amesema kwamba eneo la Geza Ulole, Kigamboni anataka kuijengea timu Uwanja wa mazoezi tu mdogo na kwamba Uwanja mkubwa na wa kisasa utakuwa Jangwani.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo makao makuu ya klabu, Jangwani, Dar es Salaam kuhusu Mkutano Mkuu wa dharula Jumapili, Manji aligusia pia baadhi ya mambo mengine ya maendeleo ya klabu
Kule Geza Ulole tutajenga Uwanja wa mazoezi na gym. Lakini Uwanja mkubwa na wa kisasa tutajenga hapa hapa Jangwani. Kama klabu za Ulaya, Uwanja wa mazoezi unakuwa tofauti na Uwanja wa mechi,”alisema.
Yanga inatarajiwa kuwa na Mkutano wa dharula Jumapili wiki hii Uwanja wa Kaunda, uliopo makao makuu ya klabu, Jangwani, Dar es Salaam na Manji amewataka wanachama kujitokeza kwa wingi kujadili mustakabali wa klabu yao.
Ajenda kuu ya Mkutano huo ni kupitisha Baraza la Wadhamini la klabu hiyo pamoja na kuondoa Mjumbe mmoja na kuweka mpya.
Na hayo yanafuatia Baraza la Wadhamini kuikodisha timu kwa kampuni ya Yanga Yetu kwa miaka 10, baada ya wanachama kuafiki ombi la Mwenyekiti wao, Yussuf Manji katika Mkutano wa Agosti 6, mwaka huu.
Pamoja na hayo, Manji amesema mzee Ibrahim Akilimali amepoteza haki ya uanachama wa klabu hiyo kwa kuwa hajalipia kadi yake kwa miezi sita iliyopita.
“Akilimali kama anataka kuja kwenye mkutano Jumapili kwanza aende kwenye tawi lake akaomba uanachama upya,” amesema Manji.
Mwenyekiti huyo amewakaribisha wale wote wanaopinga wazo lake la kuikodisha timu katika mkutano wa Jumapili, kwani kuishia kuzungumza kwenye vyombo vya Habari haitasaidia.

No comments:

Post a Comment