KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 7, 2016

TENGA MWENYEKITI WA HESHIMA CECAFA, CHALENJI KUCHEZWA SUDAN



Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
WAKATI Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) likimteua Mwenyekiti wa zamani wa baraza hilo, Leodegar Tenga kuwa mwenyekiti wa heshima, limetangaza kuwa mashindano ya mwaka huu ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge yatafanyika nchini Sudan.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye, mashindano hayo yatafanyika Sudan na tayari Wizara ya Michezo ya nchi hiyo kwa kushirikisha na Chama cha nchi hiyo (SFA) wamethibitisha kuwa wenyeji wa michuano hiyo.
Musonye alisema kuwa uamuzi wa kuipa Sudan uenyeji ulipitishwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya CECAFA kilichofanyika juzi Jumatatu mjini Khartoum kikiwa na malengo ya kupanga mikakati ya maendeleo ya ukanda huo.
Kiongozi huyo alisema kuwa pia CECAFA imeshaingia makubaliano na Chama cha Soka cha Saudi Arabia kwa ajili ya kutoa ushirikiano na baraza hilo katika kuendesha programu mbalimbali za maendeleo za soka la vijana na wanawake.
Mwenyekiti mpya wa CECAFA, Gaffar Mutasin, ambaye ni raia wa Sudan aliahidi kuendeleza soka la wanawake na vijana katika uongozi wake ili kuinua kiwango cha soka cha nchi 12 wanachama  wa baraza hilo.
CECAFA pia imeshapitisha kuwa mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) mwaka huu yatafanyika Zanzibar wakati ya vijana ya umri chini ya miaka 17 yatachezwa Uganda na Burundi itakuwa mwenyeji wa michuano ya vijana ya umri chini ya miaka 20.
Uganda ndiyo bingwa wa mashindano ya Kombe la Challenge wakati Azam FC ya Tanzania Bara ndiyo wanakishikilia kikombe cha Kagame baada ya kuwafunga Gor Mahia mwaka jana.

No comments:

Post a Comment