KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, January 1, 2016

HOYCE TEMU ATEMBELEA KAMBI YA WAZEE WASIOJIWEZA


Miss Tanzania 1999, Hoyce Temu (wa pili kushoto) akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Lino International Agency ambao ni waandaaji wa shindano la Miss Tanzania, Hashim Lundenga (katikati) kushoto Mkuu wa Itifaki wa Kamati ya Miss Tanzania, Albert Makoye ( wa pili kulia), Katibu wa Kamati ya Miss Tanzania Bosco Majaliwa (kulia) pamoja na mpiga picha wa kipindi cha Mimi na Tanzania, Geofrey Magawa a.k.a KIM (kushoto) wakiwasili Desemba 31, 2015 kwenye makazi ya wazee na watu wenye ulemavu wasiojiweza yaliyopo Nunge, Kigamboni, jijini Dar es Salaam.


Na Rabi Hume, Modewjiblog

Miss Tanzania wa mwaka 1999, Hoyce Temu amemaliza mwaka 2015 kwa kutembelea kituo Nunge ambacho ni makazi ya wazee na walemavu wasiojiweza kilichopo Vijibweni, Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Hoyce ambaye amekuwa akisaidia watu wa aina mbalimbali wenye matatizo ikiwa ni kama moja ya kazi wanazofanya mamiss kwa jamii pia kupitia kipindi chake cha Mimi na Tanzania ambacho kimekuwa kikisaidia watu mbalimbali na katika halfa hiyo aliongozana na watu wake wa karibu ikiwepo kamati ya Miss Tanzania.

Katika halfa hiyo iliyodhaminiwa na Malaika Beach, Hoyce baada ya kuwasili kituoni hapo yeye na timu nzima aliyoongozana nayo walifanya shughuli za kijamii katika kituo hicho ikiwa ni pamoja na kufanya usafi katika makazi ya wazee na walemavu wasiojiweza waliopo kituoni kwa kupulizia dawa za kuulia wadudu katika nyumba zao, kugawa dawa za mbu, maji, juice na biskuti na baadae wakapata chakula cha pamoja na wazee na walemavu wasiojiweza.

Akizungumzia halfa hiyo ya kufunga mwaka, Hoyce Temu alisema kumekuwepo na kusahaulika kwa makundi ya watu wasiojiweza na jinsi muda unavyokwenda wanazidi kusahaulika na jamii inayowazunguka.

Alisema yeye kama Miss Tanzania ana wajibu wa kujitoa kuwasaidia watu wa aina hiyo na amekuwa akifanya maeneo mengi kwa kujumuika nao kwa kuwapa msaada na kuwafariji kwani nao wana thamani kama binadamu wengine.

“Kadri inavyokwenda kumalizika karne ya 21 kunazidi kuongezeka kwa makundi ya wasiojiweza na mimi kama Miss Tanzania nimeamua kujitoa kwa kusaidia makundi haya kwani ni wajibu wetu na tukumbuke na sisi tunaelekea huko,” alisema Hoyce.

Aidha Hoyce alitoa ushauri kwa mamiss wenzake kuwa wanatakiwa kuisaidia jamii kwa kutumia fursa walizonazo mbele ya jamii kwa kutoa misaada kwa makundi ya aina mbalimbali.

Alisema kazi ya kusaidia jamii siyo ya serikali pekee na wao kama mamiss na watu wenye uwezo kwa ujumla wana wajibu wa kusaidia na sio kutazama mijini pekee kutokana na kundi kubwa la wasiojiweza kuwa vijijini.

“Sio swala la serikali pekee … ukichaguliwa kuwa mrembo unakuwa na malengo ambayo umeyaweka hivyo watumie umaarufu, sura zao na sauti kufikia watu wa aina mbalimbali ambao wanahitaji msaada, ” Na sio wazee pekee, 65% ya nchi yetu ni vijana na 20% wanajihusisha na kutumia madawa ya aina mbalimbali hivyo wanaweza kuwatembelea na kutoa elimu juu ya athari za utumiaji wa madawa hayo,” alisema Hoyce.

Nae Mkurugenzi wa Lino International Agency, ambayo ndiyo waandaji wa shindano la Miss Tanzania, Hashimu Lundenga alimtaja Hoyce kama Miss bora kuwahi kutokea tangu walipoanzisha shindano la Miss Tanzania mwaka 1994.

Alisema mamiss wengi wamekuwa wakiisaidia jamii lakini Hoyce amekuwa akijitoa zaidi kuliko wengine na kufanya shindano hilo kuonekana kuwa na faida mbele ya jamii.

“Naomba niseme ukweli Hoyce anatakiwa kuwa mfano wa kuigwa haijawahi kutokea miss aliyejitoa kusaidia jamii kama yeye na wapo wengine wanasaidia ila Hoyce amekuwa mstari wa mbele kwa hilo tunampongeza na tunamwomba azidi kuwa hivyo,” alisema Lundenga.

Kwa upande wa Afisa Mfawidhi wa kituo cha Nunge, Ojuku Mgedzi amemshukuru Hoyce kwa upendo amekuwa nao kwa kituo hicho ambacho awali aliwahi kukitembelea 2006 akiwa na marehemu Amina Chifupa na kumtaka kuzidi kuwa na moyo huo kwa jamii inayomzunguka.

Mgedzi pia alizungumzia changamoto zinazowakabili kuwa ni pamoja na kutokuwepo kwa uzio hivyo kutokuwa na hali ya usalama, kuvamiwa kwa eneo hilo na wananchi ambalo lina hekali 50.8 na tayari asilimia 50 imevamiwa na tayari taarifa ipo wizarani na wanashughulikia na zingine ndogo ndogo Hoyce akiahidi kuwasaidia.

Nae mmoja wa washiriki aliyeongozana na Hoyce, Tausi Mwenda alisema kuwa amejifunza mambo mengi kupitia halfa hiyo aliyoifanya Hoyce na kuwashauri watu wa aina mbalimbali kuwa na moyo wa kujitoa kusaidia jamii kama anavyofanya Hoyce.

Miss Tanzania 1999, Hoyce Temu akimkumbatia rafiki yake wa siku nyingi mmoja wa wazee wenye ulemavu uliotokana na ugonjwa wa ukoma, Mganga Shija (66), wakati alipotembelea makazi ya wazee na watu wenye ulemavu wasiojiweza yaliyopo Nunge, Kigamboni, jijini Dar es Salaam Desemba 31, 2015 ikiwa ni mojawapo ya shughuli ya kijamii kuuaga mwaka 2015 na kukaribisha mwaka mpya 2016.
Miss Tanzania 1999, Hoyce Temu akiendelea kufurahi na rafiki yake wa siku nyingi mmoja wa wazee wenye ulemavu uliotokana na ugonjwa wa ukoma, Mganga Shija (66), wakati alipotembelea makazi ya wazee na watu wenye ulemavu wasiojiweza yaliyopo Nunge, Kigamboni, jijini Dar es Salaam Desemba 31, 2015 ikiwa ni mojawapo ya shughuli ya kijamii kuuaga mwaka 2015 na kukaribisha mwaka mpya 2016.

No comments:

Post a Comment