KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 2, 2011

WEMA: NIMEMUOMBA RADHI BOB JUNIOR





Asema wamekubaliana kufuta kesi iliyopo mahakamani

Adai hajaachana na Diamond, amponda Chalz Baba


MREMBO wa Tanzania wa mwaka 2006, Wema Sepetu amekiri kumtusi hadharani msanii Raheem Rummy (Bob Junior) na kusema kuwa amemuomba radhi kwa kosa alilolifanya.
Wema, ambaye pia ni mwigizaji maarufu wa filamu nchini amesema, anashukuru kwamba Bob Junior amekubali kumsamehe na yupo tayari kufuta kesi aliyomfungulia mahakamani.
Mwanadada huyo mwenye vituko, alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa na kituo cha televisheni cha Clouds cha mjini Dar es Salaam.
“Naweza kusema nina furaha kwa sababu kesi imefikia sehemu nzuri. Nimemuomba msamaha (Bob Junior) na nimekiri kwake kwamba nilifanya makosa,”alisema Wema.
“Kila kitu kinakwenda vizuri. Tumeamua kusameheana. Si lazima tupelekane mbali, nimejirudi, nimekiri nimefanya kosa. Sisi sote ni vijana,”aliongeza.
Wema (26) pia alikanusha madai kuwa, ametengana na mpenzi wake wa sasa, msanii wa muziki wa kizazi kipya, Nassir Abdul ‘Diamond’ na kusisitiza kuwa, bado wapo pamoja.
“Mimi na Diamond tumeachana? Hakuna kitu kama hicho. Hatujaachana, tupo pamoja,”alisema.
Mrembo huyo wa zamani wa Tanzania pia alikanusha madai kuwa, amerejesha uhusiano wa kimapenzi kwa mpenzi wake wa zamani, mwanamuziki Chalz Baba wa bendi ya Twanga Pepeta International.
“Mungu wangu, sijarudi kwa Chalz Baba na wala sifikirii kufanya hivyo,”alisema.
Kwa mujibu wa Wema, hajawahi kukutana na Chalz na kuzungumzia kuhusu kurudiana na kuongeza kuwa, mwanamuziki huyo anavumisha habari hizo kwa lengo la kutaka kuonekana kwenye magazeti.
“Ninachokiona hapa ni kwamba anatafuta skendo kwa nguvu ili sura yake iongekane kwenye magazeti. Na kibaya zaidi, magazeti yanatumia picha za zamani tulizopiga pamoja ili kuhalalaalisha habari hizo,”alisema.
Wema alisema wakati alipokuwa na uhusiano wa kimapenzi na Chalz, taarifa zake zilikuwa zikiandikwa mara kwa mara kwenye magazeti na huenda anaikosa burudani hiyo kwa vile anapenda kuuza sura.
“Kama anatafuta kitu kingine sawa, lakini mimi na Diamond tupo pamoja, tunapendana na hatujaachana,”alisema.
Mrembo huyo alidai kuwa, Chalz amekuwa akimpigia simu mara kwa mara na kuzungumza vitu vya kijinga na kuweka sauti kwenye simu yake ili rafiki zake wamsikie atasema nini.
“Katika hili nasema wazi kuwa sitaki kurudi nyuma. Nimekuwa nikimchana laivu na kumwambia siwazii chochote juu yake. Mimi na Diamond bado tunapendana na hatutaachana,”alisema.
Msanii huyo amewataka watanzania kuacha kumtazama kwa jicho baya ama kumfikiria vibaya. Amewaomba wawe na imani juu yake kwa sababu baadhi ya watu wamekuwa wakimchafua na kumpaka matope kwa sababu wanazozijua wenyewe.
Wema (26) alipandishwa kizimbani mapema mwezi uliopita kwenye Mahakama ya Mwanzo Kinondoni Dar es Salaam kujibu shitaka la kumtukana matusi ya nguoni Bob Junior (Rais wa Masharobaro).
Akisoma shitaka hilo, karani Sharifa Dunia alidai kuwa, Aprili 11, mwaka huu, saa 12.38 jioni huko Kinondoni, Wema alimtukana Rummy.
Wema alikiri kutukana matusi hayo baada ya kuulizwa na Hakimu Mariamu kama shitaka alilosomewa ni la kweli au si kweli. Hakimu Mariam alimuuliza Wema sababu za kutukana matusi hayo, ambapo alisema ilikuwa ni kwa sababu ya hasira.
Hiyo ilikuwa mara ya tatu kwa mlimbwende huyo kufikishwa mahakamani kwa makosa mbalimbali. Alifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Februari 2009 kwa kosa la kuvunja kioo cha gari la mpenzi wake wa zamani, Steven Kanumba kilichokuwa na thamani ya sh. milioni 1.5.
Hata hivyo, kesi hiyo iliyofunguliwa kwenye Mahakama ya Kinondoni, ilifutwa baada ya pande zinazohusika kukubali kusuluhishwa nje ya mahakama.
Mwaka huo huo, Wema alipandishwa tena kizimbani kwa tuhuma za wizi wa televisheni na radio, akishirikiana na mpenzi wake, Jumbe Mohamed. Alidaiwa kuiba vifaa hivyo nyumbani kwao.
Kesi hiyo nayo ilifutwa baada ya pande zinazohusika kukubaliana kusuluhisha suala hilo nje ya mahakama.
Mbali na kujipatia sifa kutokana na kutwaa taji la Miss Tanzania mwaka 2006, Wema alianza kung’ara kwenye fani ya uigizaji baada ya kucheza sinema ya A Point of No Return, akishirikiana na Kanumba.
Sinema zingine alizocheza na kujipatia umaarufu ni pamoja na Fake Pastor, White Maria na A Diary, ambayo ameicheza kwa kushirikiana na Jackline Pentzel na Rose Ndauka kupitia kampuni yao ya Jerowe.

No comments:

Post a Comment