KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 23, 2011

BABU NJENJE AANGUA KILIO

Babu Njenje akiwa na mwimbaji mkongwe wa taarab, Shakila Saidi




Atimiza umri wa miaka 64 sanjari na Shakila Saidi

Walizaliwa tarehe moja, mwezi mmoja na mwaka mmoja

Shakila alinyonyeshwa na mama yake Babu Njenje


ILIKUWA kama sinema ama filamu ya mauzauza. Hakuna aliyeamini nini kiliandaliwa ama kingetokea nini. Lakini ndivyo ilivyokuwa.
Mwanamuziki mkongwe wa bendi ya muziki wa dansi ya The Kilimanjaro ‘Njenje’, Mabrouk Hamisi wiki iliyopita alijikuta akitokwa machozi bila kutarajia baada ya kituo cha radio cha Clouds kuandaa kitu, ambacho kilimstaajabisha kama sio kumwacha hoi.
Siku hiyo, mtangazaji wa kipindi cha Leo Tena cha Clouds, Dina Marios alimwalika studio mwanamuziki huyo maarufu kwa jina la Babu Njenje kwa kile alichomweleza kuwa ni kurekodi naye kipindi. Babu Njenje alifika studio za Clouds akiwa na wanamuziki wenzake, akijua ni mahojiano ya kawaida. Kumbe kulikuwa na mpango maalumu wa kumshangaza. Siku hiyo ilikuwa ni siku ya kuzaliwa kwake. Alitimiza umri wa miaka 65.
Ilichokifanya Clouds ni kumshangaza mwanamuziki huyo. Kituo hicho kilianza kupiga nyimbo mbalimbali za Kilimanjaro kisha Babu Njenje akapigiwa wimbo wa kumpongeza wa ‘Happy birthday to you’.
Baada ya wimbo huo, Clouds ikamuunganisha Babu Njenje kwa njia ya simu na familia yake iliyokuwa mjini London, Uingereza bila yeye kutarajia.
Familia yote ya Babu Njenje ipo nje ya nchi. Mkewe anaishi Marekani pamoja na mtoto wake wa kwanza wa kiume, Feisal. Mtoto wake wa kike, Lulu anaishi Uingereza. Babu Njenje anao wajukuu wanne.
Katika mazungumzo hayo, familia ya Babu Njenje ilimtakia kila la heri katika siku hiyo muhimu kwake
Babu Njenje alilia sana na akasema hajawahi kushangazwa na kitu chochote katika maisha yake yote, siku hiyo ilikuwa kiboko. Mara zote alipokuwa akizungumza na familia yake, alijitahidi kujizuia kulia, lakini ilikuwa vigumu.
Babu Njenje na mkewe wote wamezaliwa tarehe na mwezi mmoja. Siku hiyo hiyo, mkewe naye alikuwa akitimiza miaka 60. Bila kujua kwamba Clouds ilishafanya mawasiliano na mkewe kwa njia ya simu, kwake kumsikia ilikuwa ni kama miujiza. Hakuamini.
Dina anasema alikaa na mwanamuziki Waziri Ally wa The Kilimanjaro na kuamua kupanga tukio hilo dogo kwa vile si jambo zuri kumuenzi mwanamuziki baada ya kufa.
Babu Njenje amekuwa na bendi ya The Kilimanjaro kwa miaka zaidi ya 38. Awali, bendi hiyo ilikuwa ikijulikana kwa jina la The Revolution kabla ya kubadili jina na kuitwa The Kilimanjaro. Lakini kwa sasa ni maarufu zaidi kwa jina la Njenje kutokana na wimbo uliobeba jina hilo.
Siku hiyo hiyo, Clouds pia ilikuwa imemwalika mkongwe wa muziki wa taarab nchini, Shakila Said. Wakongwe hao wawili, kila mmoja hakuna aliyetarajia iwapo wangekutana ndani ya studio ya kituo hicho.
Lengo la Clouds kuwakutanisha wakongwe hao ni kwa sababu wana historia inayofanana na tena yenye mvuto.
Babu Njenje na Shakila walizaliwa siku moja, tarehe moja, mwezi mmoja na mwaka mmoja. Mitaa waliyokuwa wakiishi ilikaribiana. Kutoka kwa Babu Njenje kwenda kwa Shakila ni umbali wa nyumba nne.
Babu Njenje alizaliwa asubuhi na Shakila alizaliwa jioni. Mama yake Shakila hakuwa na maziwa ya kutosha kumnyonyesha, hivyo ikabidi apelekwe kwa mama yake Babu Njenje kunyonya.
Wasanii hawa wawili wamekuwa pamoja, wamecheza pamoja na walianza kusoma madrasa pamoja. Siku hiyo kila mmoja alikuwa anatimiza umri wa miaka 65.
Haikuwahi kutokea hata mara moja kwa wakongwe hao kusherekea siku zao za kuzaliwa pamoja. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza. Hongera Clouds.
Ilibidi Shakila apewe nafasi ya kuimba nyimbo zake mbalimbali za zamani. Kiukweli sauti yake bado ni maridhawa, licha ya umri wake mkubwa. Ni sauti adhimu. Mola aendelee kumpa afya njema.
Wote wawili bado wanatesa katika anga la muziki. Shakila ni mwimbaji mwalikwa katika kikundi cha sanaa za maonyesho cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Mbali ya sherehe hiyo ndogo, bendi ya The Kilimanjaro nayo ilimwandalia tafrija ndogo Babu Njenje kwa lengo la kumuenzi. Sherehe hiyo ilifanyika kwenye ukumbi wa Salender Bridge.
Siku hiyo, Lulu aliwasili ukumbini ghafla bila Babu Njenje kuwa na taarifa. Alikuwa ametokea Uingereza. Walikuwa hawajakutana kwa miaka mingi. Yalikuwa maajabu makubwa kwa Babu Njenje kumuona Lulu ukumbini siku hiyo.
Lulu alipewa kipaza sauti na kuanza kuimba wimbo wa Happy birthday. Aliimba wimbo huo huku akiwa anaelekea stejini, ambako baba yake alikuwa amesimama, akiwa hajui hili wala lile.
Babu Njenje alionekana kushangaa. Hakuwa anaelewa nini kinatokea. Walipokaribiana, wakakumbatiana kwa furaha ya ajabu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa sherehe ya Babu Njenje kutimiza miaka 65.

No comments:

Post a Comment