KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, November 12, 2013

BODI YA LIGI YAFUNGIA VIWANJA SABA, SIMBA NA MBEYA CITY ZATOZWA FAINI


 
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPL Board) imefungia viwanja saba vilivyokuwa vikitumiwa na timu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) hadi vitakapofanyiwa marekebisho ili kukidhi mahitaji ya mechi za mpira wa miguu.
 
Uamuzi huo umefikiwa na TPL Board katika kikao chake cha kwanza kilichofanyika juzi (Novemba 10 mwaka huu) jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine kilipitia ripoti za mechi za VPL na FDL katika mzunguko wa kwanza.
 
Viwanja vilivyofungiwa na marekebisho yanayotakiwa kufanyika kwanza ili viruhusiwe kutumika tena ni Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba (majukwaa yake yamechakaa, hivyo kuhatarisha usalama wa watazamaji), na Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga (vyumba vya wachezaji kubadilishia nguo (dressing rooms) havina hadhi).
 
Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya (sehemu ya kuchezea- pitch ni mbovu), Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha (pitch ni mbovu), Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi (vyumba vya kubadilishia kutumika kwa ajili ya shule ya awali), Uwanja wa Majimaji mjini Songea (pitch ni mbovu) na Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro (pitch ni mbovu).
 
Klabu ambazo timu zake zinatumia viwanja hivyo zimeshaarifiwa rasmi juu ya uamuzi huo ambapo ama vinatakiwa kuwasiliana na wamiliki wa viwanja hivyo ili wafanye marekebisho au kutafuta viwanja vingine vya kuchezea mechi zao.
 
Kwa upande wa ripoti za mechi za VPL; Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 na kupewa onyo kali kwa timu yake ya U20 kutocheza mechi ya utangulizi walipocheza na Yanga. Pia wanatakiwa kulipa gharama za uharibifu baada ya washabiki wao kuvunja kioo cha basi la Yanga baada ya gharama hizo kuthibitishwa na Bodi ya Ligi.
 
Pia Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa washabiki wake kushambulia basi la wachezaji wa Tanzania Prisons baada ya mechi dhidi yao, na kulipa gharama za uharibifu baada ya kuthibitishwa na Bodi ya Ligi.
 
Coastal Union imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake ilipocheza na Azam kwenye Uwanja wa Mkwakwani ambapo mwamuzi msaidizi Hassan Zani alishambuliwa kwa mawe na kujeruhiwa mkononi na kichwa, tukio lililosababisha mchezo kusimama kwa dakika tatu.
 
Beki wa Coastal Union, Hamad Khamis wa  amepigwa faini ya sh. 500,000 kwa kumpiga kichwa kwa makusudi Kipre Tchetche wa Azam. Kitendo hicho kilisababisha refa amtoe nje kwa kadi nyekundu, hivyo atakosa mechi tatu zinazofuata za timu yake.
 
Mchezaji Cosmas Lewis wa Ruvu Shooting alifanya kitendo cha utovu wa nidhamu kwa kupiga kelele wakati mgeni rasmi akisalimia timu na kukataa kupeana mkono na kamishna kwenye mechi dhidi ya Rhino Rangers, hivyo amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000.
 
Mtunza vifaa (Kit Man) wa JKT Ruvu, Selemani Oga aliondolewa kwenye benchi la ufundi wakati wa mechi yao dhidi ya Mbeya City kwa kosa la kutoa lugha chafu kwa refa, hivyo suala lake litapelekwa katika Kamati ya Maadili.
 
Kocha Msaidizi wa Oljoro JKT, Fikiri Elias amepigwa faini ya sh. 500,000 na kufungiwa mechi tatu kwa kumshambulia kwa matusi refa wakati wa mechi yao dhidi ya Ashanti United. Naye mtunza vifaa wa timu hiyo Elas Justin amepelekwa Kamati ya Maadili kwa kumshambulia refa kwa matusi ya nguoni.
 
Simba wamepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake wakati wa mechi dhidi ya Kagera Sugar.
 
Katika FDL, mchezaji Ally Mtoni wa Villa Squad amepigwa faini y ash. 200,000 na kufungiwa mechi tano. Kosa lake ni kujisaidia haja ndogo golini wakati wa mechi dhidi ya Ndanda FC iliyochezwa mjini Mtwara.
 
Kamishna Paul Opiyo wa mechi ya FDL kati ya Villa Squad na Transit Camp amepewa onyo wa kutokuwa makini. Katika ripoti yake ameeleza kuwa Transit Camp ilichelewa kufika uwanjani, lakini hakusema ilichelewa kwa muda gani.
 
Kocha wa Polisi Dar es Salaam, Ngelo Nyanjabha na Meneja wa timu hiyo Mrimi Masi wamepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi tatu kila mmoja kwa kuongoza kundi la washabiki kumvamia refa wa mechi yao dhidi ya Villa Squad iliyochezwa Dar es Salaam.
 
Pia Bodi ya Ligi imeagiza Polisi waandikiwe barua ya onyo kwa vile wakati waamuzi wanapigwa walikuwepo, lakini hawakutoa msaada kwa wakati.
 
Kocha wa Friends Rangers, Kheri Mzozo amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi sita kwa kosa la kumtukana refa na kutishia kuhamamisha washabiki waingie uwanjani kufanya fujo kwenye mechi dhidi ya Villa Squad.
 
Naye Kocha msaidizi wa timu ya Transit Camp, Haji Amiri amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi sita kwa kutoa lugha ya matusi kwa mwamuzi wa akida wakati wa mechi dhidi ya Friends Rangers.
 
Adhabu zote zimetolewa kwa mujibu wa kanuni. Pia Bodi ya Ligi imeahirisha kufanya uamuzi wa mechi kati ya Stand United na Kanembwa JKT iliyochezwa Uwanja wa Kambarage ili kukusanya taarifa zaidi. Mechi hiyo haikumalizika. Bodi ya Ligi itakutana tena Jumapili (Novemba 17 mwaka huu).
 
FUTURE TAIFA STARS vs TAIFA STARS UWANJANI KARUME KESHO
Timu za Taifa za Future Taifa Stars na Taifa Stars zinacheza kesho (Novemba 13 mwaka huu). Mechi hiyo ya kirafiki itafanyika Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.
 
Mechi hiyo ni maalumu kwa Benchi la Ufundi la Taifa Stars linaloongozwa na Kim Poulsen kuangalia wachezaji kumi kutoka Future Taifa Stars watakaoongezwa katika Taifa Stars tayari kwa mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayochezwa Novemba 19 mwaka huu jijini Arusha.
 
Watazamaji 300 tu wataruhusiwa kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000.
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imeingia kambini leo (Novemba 12 mwaka huu). Miongoni mwa wachezaji wanaotarajia kuripoti ni kipa Ivo Mapunda wa Gor Mahia.
Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania

No comments:

Post a Comment