KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, November 3, 2013

AZAM, MBEYA CITY ZAISHUSHA YANGA KILELENI MWA LIGI



AZAM FC imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 3-0 hii leo dhidi ya Ruvu Shooting, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.


Ushindi huo, unaifanya Azam itimize pointi 36 baada ya kucheza mechi 12, hivyo kuwashusha Yanga SC waliokuwa kileleni kwa pointi 25 baada ya ushindi wa jana wa 3-0 dhidi ya JKT Ruvu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Jabir Aziz kulia na Erasto Nyoni wakimpongeza Khamis Mcha 'Vialli' kufunga bao la tatu

Hadi mapumziko, Azam FC walikuwa mbele kwa mabao 2-0 yaliyowekwa kimiani na Kipre Tchetche na kinda Joseph Kimwaga aliyepandishwa kutoka akademi msimu huu.

Kipre alifunga bao tamu dakika ya kwanza tu ya mchezo, baada ya kuwatoka wachezaji wa Ruvu Shooting kuanzia katikati ya Uwanja na kuingia kwenye eneo la mita 18 kupiga shuti lililotinga nyavuni.

Kimwaga aliyefunga bao la tatu katika ushindi wa 3-2 dhidi ya Yanga mwezi uliopita, leo alifunga bao lake dakika ya 45 akiunganisha kwa kichwa krosi ya beki wa kushoto, Waziri Salum.

Pamoja na kufungwa, Ruvu Shooting inayofundishwa na Charles Boniface Mkwasa, ndiyo iliyotawala mchezo kipindi cha kwanza na kama si uimara wa kipa Mwadini Ally kuokoa michomo ya hatari, wangepata mabao.

Kipindi cha pili, Azam waliendelea kucheza kwa umakini na hesabu za kusaka mabao zaidi, huku Ruvu wakiendelea kucheza kufurahisha majukwaa na haikuwa ajabu dakika ya 70, Azam walipopata bao la tatu.

Bao hilo lingine zuri katika mchezo wa leo, lilifungwa na Khamis Mcha ‘Vialli’ kwa shuti kali baada ya kumtoka beki wa Ruvu Shooting.

Timu ya bilionea, Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa, Azam sasa itakamilisha mzunguko wa kwanza kwa kumenyana na Mbeya City Novemba 7, mechi ambayo inatarajiwa kuwa kali na ya kusisimua kutokana na timu zote kukabana kileleni pamoja na Yanga.

Kikosi cha Azam FC leo kilikuwa; Mwadini Ally, Erasto Nyoni, Waziri Salum, Said Mourad, Aggrey Morris, Kipre Balou, Khamis Mcha, Himid Mao/Jabir Aziz dk58, Kipre Tchetche, Humphrey Mieno na Joseph Kimwaga/Farid Mussa dk69.

Ruvu Shooting; Abdul Seif, Michael Pius, Stefano Mwasyika, Mangasini Mbonosi, Shaaban Suzan, Juma Dion, Juma Nade, Hassan Dilunga, Saidi Dilunga, Elias Maguri na Cossmas Lewis

Wakati huo huo, Mbeya City imerejea nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo baada ya kuichapa Ashanti bao 1-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Ushindi huo umeiwezesha Mbeya City kuwa na pointi sawa na Azam, lakini zinatofautiana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.

No comments:

Post a Comment