KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, February 14, 2015

YANGA YAJIWEKA PAZURI MICHUANO YA AFRIKA


MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Burundi, Amisi Joselyn Tambwe leo ameibuka shujaa, baada ya kuifungia timu yake mabao yote mawili ikishinda 2-0 katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Awali Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya BDF XI ya Botswana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ushindi huo, unaiweka Yanga SC katika mazingira mazuri ya kuingia hatua ya 32 Bora, ambako itamenyana na mshindi kati ya Sofapaka ya Kenya na Platinum ya Zimbabwe.

Tambwe alifunga bao la kwanza dakika ya kwanza tu kwa kichwa kufuatia krosi maridhawa ya winga Simon Msuva, ambaye alimtoka vizuri beki wa kulia wa BDF, Pelontle Lerole.

Baada ya bao hilo, Yanga SC ilitengeneza nafasi zaidi ya tatu nzuri, lakini ikashindwa kufunga. Kipindi cha pili, Yanga SC walirudi vizuri tena na kuendelea kusukuma mashambulizi langoni mwa BDF.

Hali hiyo ilizaa matunda dakika ya 55 baada ya Tambwe tena kufunga kwa kichwa akimalizia pasi nzuri ya Mrisho Khalfan Ngassa aliyempiga chenga beki wa BDF, Mompati Thuma.

Yanga SC waliendelea kulisakama lango la BDF, ambayo ilikuwa ikifanya mashambulizi ya kushitukiza yasiyo na madhara, lakini hawakufanikiwa kupata mabao zaidi. 

Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Salum Telela, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amisi Tambwe/Jerry Tegete dk82, Mrisho Ngassa na Andrey Coutinho/Kpah Sherman dk70.

BDF XI; Tukudzwa Ndoro, Pelontle Lerore, Othusitse Mpharitlhe, Kelegeste Mogomotsi, Mombati Thuma, Mosha Gaolaolwe, Master Masitara, Bonolo Phuduhudu, Vincent Nzombe/Kumbulani Madziba dk76, Thato Ogopotse na Kabelo Seakanyeng.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BINZUBEIRY.

No comments:

Post a Comment