KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, February 8, 2015

YANGA MWENDO MDUNDO



MSHAMBULIAJI Mrisho Ngasa jana aliibuka shujaa wa Yanga baada ya kuifungia mabao mawili katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar.

Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga iliichapa Mtibwa Sugar mabao 2-0 na kurejea kileleni mwa ligi hiyo.

Mechi hiyo ilikuwa ya kwanza kwa Ngasa tangu aliporejea nchini kutoka Afrika Kusini, alikokwenda kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa.

Ngasa alifunga mabao hayo katika kipindi cha pili baada ya kuingia uwanjani kuchukua nafasi ya Kpah Sherman.

Mshambuliaji huyo aliyewahi kuzichezea Azam na Simba, alifunga bao la kwanza dakika ya 55 baada ya kupokea pasi maridhawa kutoka kwa Simon Msuva.

Nyota huyo wa timu ya taifa, Taifa Stars, aliongeza bao la pili dakika ya 62 baada ya kuwachambua mabeki wa Mtibwa kabla ya kufumua shuti lililompita kipa Said Mohamed.

Ushindi huo wa Yanga ni wa pili mfululizo na umekuja siku chache baada ya kuichapa Coastal Union bao 1-0 wiki iliyopita mjini Tanga.

No comments:

Post a Comment