KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, June 5, 2013

Rooney ampasua kichwa Wenger



LONDON, England
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa England, Wayne Rooney amewaweka roho juu mashabiki wa klabu ya Manchester United baada ya kukiri hadharani kwamba, anaweza kuondoka Old Trafford msimu huu.

Kauli hiyo ya Rooney imemfanya Kocha Mkuu wa Arsenal, Arsene Wenger awe tayari kuvunja benki na kuweka rekodi ya kumsajili nyota huyo kwa bei mbaya.

Wenger alisema wiki hii kuwa, hawezi kupoteza nafasi adhimu ya kumsajili mshambuliaji huyo, ambaye anaonekana kutofurahia uwepo wake Old Trafford.

Rooney (27) aling'ara mwishoni mwa wiki iliyopita, ikiwa ni pamoja na kuifungia bao England ilipomenyana na Brazil na kutoka nayo sare ya mabao 2-2 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa kwenye uwanja wa Maracana.

Mwezi uliopita, gazeti la Daily Mail la Uingereza liliripoti kuwa, Arsenal imepata uhakika mkubwa wa kumsajili Rooney baada ya mchezaji huyo kusema kuwa, anataka kuondoka Old Trafford.

Tayari Wenger ameshaweka wazi kuwa, yuko tayari kuvunja rekodi ya kumsajili nyota huyo wa zamani wa klabu ya Everton.

"Rooney ni mchezaji, ambaye anamvutia kila mtu duniani, nani anayeweza kukataa kumsajili," Wenger alikieleza kituo cha televisheni cha Al Jazeera wiki hii.

Wakati Wenger akihaha kumsajili nyota huyo, Kocha Mkuu mpya wa Manchester United, David Moyes anakabiliwa na kazi nzito ya kumshawishi Rooney abaki Old Trafford.

Moyes alikaririwa hivi karibuni akisema kuwa, angependa kumuona Rooney akiendelea kuitumikia Manchester United chini yake kwa vile ni miongoni mwa wachezaji muhimu.

Rooney amekuwa hana uhakika wa namba Manchester United tangu ilipomsaili Robin van Persie. Mholanzi huyo amekuwa akicheza nafasi ya mshambuliaji wa kati, ambayo Rooney alikuwa akiicheza kabla ya ujio wake.

Mapema 2010, Rooney alitishia kuihama Manchester United kabla ya Sir Ferguson kufanikiwa kumtuliza na kumuongezea mkataba mpya.

Msimu huu, Ferguson alimweka benchi Rooney wakati Manchester United iliporudiana na Real Madrid ya Hispania katika michuano ya ligi ya mabingwa wa Ulaya. Badala yake, Ferguson aliwachezesha Van Persie na Danny Welbeck katika nafasi ya ushambuliaji.

Mbali na kumwania Rooney, Wenger pia amepania kumrejesha kiungo wake wa zamani, Cesc Fabregas, ambaye alihama Emirates msimu uliopita na kujiunga na Barcelona ya Hispania.

Wenger anaamini kuwa, mpango wake wa kumrejesha Fabregas hautakuwa mgumu kutokana na mchezaji huyo kutokuwa na uhakika wa namba ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza cha Barcelona.

Kwa mujibu wa makubaliano yaliyofikiwa wakati Fabregas alipojiunga na Barcelona 2011, Arsenal inaweza kumrejesha mchezaji huyo kwa malipo kidogo ya pauni milioni 20.

"Nafikiri kwa sasa amepoteza uhakika wa namba ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza cha Barcelona,"alisema Wenger alipokuwa akimuelezea mchezaji huyo.

Wenger alimwelezea Fabregas kuwa ni mchezaji mwenye utulivu na kiwango cha juu cha soka, hivyo anaumia moyoni kwa kutopata nafasi ya kuichezea timu hiyo.

Hata hivyo, Wenger anaweza kukumbana na upinzani mkali kutoka kwa Manchester City, Manchester United na Chelsea katika kinyang'anyiro cha kumsajili nyota huyo wa England.

Kuna habari kuwa, klabu hizo tatu nazo zimekuwa zikimuwinda kwa udi na uvumba Fabregas kwa lengo la kuziongezea nguvu katika msimu ujao wa ligi.

Fabregas anatarajiwa kukutana na Kocha Mkuu wa Barcelona, Tito Vilanova wiki hii kwa ajili ya kuzungumzia mustakabali wake.

Marafiki wa karibu wa Fabregas wanaamini kuwa, kiungo huyo anaweza kuamua kubaki Barcelona iwapo atahakikishiwa namba ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza.

Kwa upande wake, Moyes amemtaja Fabregas kuwa ni mmoja wa wachezaji, ambao amepanga kuwasajili kwa lengo la kukiongezea nguvu kikosi chake.

Moyes, ambaye amerithi mikoba ya kocha wa zamani wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, anatarajiwa kuanza rasmi kibarua cha kuinoa timu hiyo Juni 16 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment