KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 13, 2013

IVORY COAST KUTUA DAR LEO USIKU



SHIRIKISHO la Soka la Dunia (FIFA) limewateua waamuzi kutoka Algeria kuchezesha mechi kati ya timu ya Taifa, Taifa Stars na Ivory Coast.

Timu hizo mbili zinatarajiwa kumenyana Jumapili katika mechi ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 204 itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema jana kuwa, waamuzi walioteuliwa kuchezesha mechi hiyo ya kundi C wataongozwa na Charef Mehdi Abid atakayekuwa mwamuzi wa kati.

Aliwataja waamuzi wengine kuwa ni Hamza Hammou na Bouabdallah Omari wakati mwamuzi wa akiba atakuwa Sofiane Bousseter.

Wambura alisema Abdi na wezake wanatarajiwa kutua nchini kesho saa 12 asubuhi kwa ndege ya Shirika la Ndege la Misri (EgyptAir).

Aliongeza kuwa mtathmini wa waamuzi wa mechi hiyo atakuwa Athanase Nkubito kutoka Rwanda, ambaye naye atatua nchini kesho saa 12 jioni kwa ndege ya RwandAir.

Alisema kamishna wa mechi hiyo ni Bernard Mfubusa kutoka Burundi, ambaye anatarajiwa kuwasili nchini kesho saa 3.35 asubuhi kwa ndege ya Kenya Airways.

Kwa mujibu wa Wambura, maofisa wote watakaosimamia mechi hiyo wanatarajiwa kuondoka nchini Jumatatu kurejea kwao.

Wakati huo huo, msafara wa timu ya Taifa ya Ivory Coast (The Elephants) utakaokuwa na watu 80, wakiwemo wachezaji 27, unatarajiwa kuwasili nchini leo kwa ndege maalumu.

Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema jana kuwa, kikosi hicho kitawasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam saa 2.50 usiku na kitafikia hoteli ya Bahari Beach iliyoko nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Wambura, nahodha wa zamani wa Ivory Coast, Didier Drogba ameachwa kwenye msafara huo.

Aliwataja Wachezaji watakaokuwemo kwenye kikosi hicho kuwa ni Abdoul Razak, Akpa Akpro Jean-Daniel Dave Lewis, Angoua Brou Benjamin, Arouna Kone, Aurier Serge Alain Stephane, Bamba Souleman, Barry Boubacar, Boka Etienne Arthur, Bolly Mathis Gazoa Kippersund, Bony Wilfried Guemiand, Cisse Abdoul Karim, Diarrassou Ousmane Viera na Dja Djedje Brice Florentin.

Wengine ni Doumbia Seydou, Gbohouo Guelassiognon Sylvain, Gosso Gosso Jean-Jacques, Kalou Salomon Armand Magloire, N’dri Koffi Christian Romaric, Sangare Badra, Serey Die Gnonzaroua Geoffroy, Sio Giovanni, Tiote Cheik Ismael, Toure Yaya Gnegneri, Traore Lacina, Ya Konan Didier, Yao Kouassi Gervais na Zokora Deguy Alain Didier.

Katika hatua nyingine, kiingilio cha chini katika mechi kati ya Taifa Stars na Ivory Coast kitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani.

Viti vya kijani katika uwanja huo wenye uwezo wa kumeza watazamaji 60,000 viko 19,648. Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu, ambavyo viko 17,045, kiingilio kitakuwa sh. 7,000. Kiingilio kwa viti vya rangi ya chungwa, ambavyo viko 11,897 ni sh. 10,000.

Viingilio vya daraja la juu ni sh. 15,000 kwa VIP C,sh. 20,000 kwa VIP B na sh. 30,000 kwa VIP A.

No comments:

Post a Comment