KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, June 3, 2013

NSSF ALL STARS YAVUNJA MWIKO WA BUNGE SC


Meneja wa timu ya NSSF All Stars, Rashid Zahor (wa pili kulia) akiwa ameshikilia kombe la ubingwa baada ya kuibuka na ushindi dhidi ya Wabunge katika mechi iliyochezwa juzi kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.
Wachezaji wa timu za soka na netiboli za NSSF All Stars wakiwa katika picha ya pamoja na vikombe walivyoshinda.
Wachezaji wa timu za soka za NSSF All Stars na Bunge SC wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mechi kati yao iliyochezwa juzi kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.
Kikosi cha timu ya soka ya NSSF All Stars kabla ya kucheza mechi yake ya kirafiki dhidi ya Bunge SC.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

TIMU ya soka ya kombaini ya vyombo vya habari, iliyoundwa kutokana na mashindano ya Kombe la Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), NSSF All Stars juzi iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Wabunge katika mechi ya kirafiki iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Ushindi huo uliiwezesha NSSF Media Stars kuvunja mwiko wa timu ya soka ya wabunge wa kutofungwa katika mechi za kirafiki inazocheza kwenye uwanja huo dhidi ya timu za taasisi mbalimbali.

Wakati NSSF All Stars iliibuka na ushindi katika soka, dada zao walipigwa mweleka wa mabao 38-11 na Wabunge. Mechi zote mbili zilionyeshwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha Star TV.

Kutokana na ushindi huo katika soka, NSSF All Stars ilikabidhiwa kombe la ubingwa na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai. Kombe hilo lilipokelewa na nahodha wa NSSF All Stars na nahodha wa timu hiyo, Majuto Omary.

Kwa upande wa Wabunge, kombe la ushindi wa pili lilipokelewa na nahodha wake,Ahmed Ngwali.

Katika netiboli,kombe la ubingwa lilipokelewa na nahodha wake, ....wakati kombe la ushindi wa pili kwa NSSF All Stars lilipokelewa na nahodha Lulu Habibu.

Mara baada ya kupokea vikombe vyao, wachezaji wa timu zote mbili za NSSF All Stars walivikabidhi kwa Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Dk. Ramadhani Dau na kisha kupiga naye picha ya pamoja.

Timu ya soka ya NSSF All Media Stars ilionyesha dhamira ya ushindi tangu mwanzo wa mchezo kutokana na kufanya mashambulizi mfululizo kwenye lango la wabunge lililokuwa chini ya Iddi Azzan.

Majuto nusura aifungie bao NSSF All Stars dakika ya 15 wakati alipofumua shuti la mpira wa adhabu wa umbali wa mita 25, lakini liligonga mwamba wa pembeni wa goli na kurudi uwanjani kabla ya kuokolewa na mabeki wa Wabunge.

Dakika 10 baadaye, Julius Kihampa aliiandikia NSSF All Stars bao pekee na la ushindi baada ya kuunganisha wavuni kwa kichwa krosi maridhawa kutoka kwa Majuto.

Zikiwa zimesalia dakika 10 kabla ya mapumziko, kipa Azzan wa wabunge alilazimika kufanyakazi ya ziada kupangua shuti la Majuto, ambapo mpira ulimtoka mikononi kabla ya kuudaka tena. Timu hizo zilikwenda mapumziko NSSF All Stars ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Katika kipindi cha pili, timu zote mbili zilifanya mabadiliko kadhaa ya wachezaji. Wabunge waliwatoa Faki Haji Makame, Adam Malima, Athumani Mfutakamba na Ahmed Ngwali na kuwaingiza Mussa Elisha, Michael Kadebe, Onesmo Laulau na Suleiman Jafu.

Kwa upande wa NSSF All Stars, iliwapumzisha Linus Bwegego, Maulid Kitenge, Julius Kihampa na Edward Mbaga na kuwaingiza Mohamed Mharizo, Nassoro Nassoro, Ridhiwani Ramadhani na Salum Mkandemba.

Katika kipindi hicho, Wabunge walichachamaa na kulishambulia lango la NSSF All Stars mara kadhaa, lakini uimara wa mabeki Mbozi Katala, Heri Mselemu na kipa Saidi Ambua uliikosesha mabao.

George Balibojani alipata nafasi nzuri ya kuifungua bao Bunge dakika ya 65 alipoingia na mpira ndani ya 20, lakini shuti lake lilitoka pembeni ya lango.

Kipa Ambua wa NSSF alilazimika kufanyakazi ya ziada dakika ya 79 baada ya kuokoa shuti la Michael Kadebe aliyekuwa katika nafasi nzuri ya kuifungia bao Bunge.

Akizungumza baada ya pambano hilo, Kocha wa NSSF All Stars, Sanifu Lazaro aliwapongeza vijana wake kwa kucheza vyema na kufuata vyema maelekezo yake na hatimaye kuibuka na ushindi.

"Vijana wamecheza vizuri sana. Tulifanya mazoezi kwa siku tatu tu kabla ya kuja Dodoma, lakini wameweza kucheza kwa kufuata maelekezo niliyowapa,"alisema.

Kocha wa Bunge, Patrick Amri alisema hawakuwa na bahati kwa vile walipata nafasi kadhaa nzuri za kufunga mabao, lakini walishindwa kuzitumia vyema. Pia alisema bao walilofungwa lilitokana na mabeki wake kutokuwa makini.   Nkumba, Jenista, Lusinde waonyesha vibweka uwanjani
MBUNGE wa Jimbo la (Sikonge), Saidi Nkumba juzi alikuwa kivutio cha aina yake kwa mashabiki baada ya kuingia uwanjani akiwa amevaa shuka nyeupe na nyekundu na kuvaa baraghashia huku akiwa ameshika usinga na kujifunga kitambaa kichwani.

Tukio hilo lilitokea wakati wa mapumziko ya pambano la soka la kirafiki kati ya Bunge na kombaini ya vyombo vya habari 'NSSF All Stars' lililofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini hapa.

Nkumba aliyeingia uwanjani kwa gari lake, alipokewa kwa mbwembwe nyingi na mbunge wa Peramiho, Jenista Mhagama na mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde.

Akiongozana na wabunge hao wawili, Nkumba alikwenda nao katikati ya uwanja huku akipunga usinga hewani na baadaye kutoka nje, ambako alisalimiana na wachezaji wa Bunge kwa kuwashika vichwa.

Tukio hilo lilishangiliwa kwa mayowe mengi na wabunge waliokuwa wamefurika kwenye uwanja huo kabla ya wachezaji wa timu ya netiboli ya NSSF All Stars kujibu mapigo kwa kuingia uwanjani na kwenda kwenye eneo la mzunguko, ambako walilizunguka wakiigiza kufanya kafara.

Wakati kipindi cha pili cha pambano hilo kikiendelea, Nkumba alikwenda kusini mwa uwanja karibu na kibendera, ambako alisimama kwa muda wote wa mchezo akipiga simu na kupunga usinga wake hewani.

Akizungumza kabla ya washindi kukabidhiwa zawadi, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhani Dau alisema waliamua kuandaa pambano hilo kwa lengo la kusherehekea miaka 10 ya mashindano ya Kombe la NSSF.

Alisema mashindano hayo, ambayo yamekuwa yakifanyika kwa ufanisi mkubwa, yamelenga kuwakutanisha wafanyakazi wa vyombo mbalimbali vya habari nchini kwa lengo la kufahamiana na kuiweka miili yao katika afya nzuri.

Dk. Dau alisema lengo la shirika lake ni kuhakikisha kuwa, mashindano hayo yanaendelea kufanyika kila mwaka na kwa ufanisi mkubwa na kwamba wamepanga kuzidi kuyaboresha kwa zawadi na kiuendeshaji.

Kwa upaande wake, mgeni rasmi katika pambano hilo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Job Ndugai aliipongeza NSSF kwa kuandaa mechi hizo mbili na kuwataka wabunge na wana habari kuendelea kuimarisha uhusiano mzuri uliopo kati yao.

Meneja wa NSSF All Stars, ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya Kombe la NSSF, Rashid Zahor alisema vijana wake wameifurahia safari hiyo na pia kupata nafasi ya kucheza na wabunge.

Zahor alisema ziara hiyo pia imewawezesha vijana wake kujifunza mengi, ikiwa ni pamoja na kukutana na baadhi ya wabunge, ambao hawakuwa wakiwafahamu.

Timu za NSSF All Stars ziliwasili Dodoma, Mei 31 mwaka huu kwa mabasi mawili ya kukodisha na kurejea Dar es Salaam jana. Msafara wa timu hizo uliongozwa na Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa NSSF, Juma Kintu.

No comments:

Post a Comment