KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, June 5, 2013

NASEEB ABDUL 'DIAMOND' : NATAKA KUWA MSANII WA KIMATAIFA



MSANII nyota wa muziki wa kizazi nchini, Naseeb Abdul 'Diamond' amesema kiwango chake cha chini cha malipo kwa kila onyesho analofanya nje ya nchi ni dola 10,000 za Marekani (sh. milioni 16).

Akihojiwa katika kipindi cha Take One Action kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha Clouds wiki hii, Diamond alisema katika baadhi ya nchi, kiwango chake cha malipo kwa kila onyesho ni kati ya dola 15,000 (sh. milioni 24) na 25,000 (sh. milioni 42)

"Sifanyi shoo nje ya nchi chini ya dola 10,000. Katika nchi kama Muungano wa Falme za Kiarabu (UAE), kiwango changu ni dola 25,000. Wakati mwingine nalipwa hadi dola 30,000,"alisema msanii huyo.

Diamond alisema katika nchi kama vile Comoro, ambako anatarajia kwenda kufanya onyesho mwishoni mwa mwezi huu, malipo yake kwa onyesho ni dola 25,000.

Hata hivyo, Diamond alisema wakati mwingine amekuwa akilipwa pesa nyingi kuliko alivyotarajia na alitoa mfano wa Rwanda, ambako promota aliyemwalika huko alimlipa sh. milioni 180,000.

"Mimi nina msimamo na ninapoalikwa nje ni lazima nifuatane na wacheza shoo wangu. Wapo wasanii wengine wa Tanzania wanaomba waende Ulaya wakafanye shoo bure kwa sababu tu hawajakwenda huko siku nyingi,"alisema.

Diamond alisema lengo kubwa alilonalo kwa sasa ni kuwa msanii wa kimataifa na amefikia uamuzi huo kutokana na funzo kubwa alilolipata wakati wa ziara yake nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

Ili kutimiza azma yake hiyo, Diamond alisema ameanza kuandika mashairi yenye mvuto, kurekodi nyimbo zake kwenye studio za kisasa na pia kutengeneza video zenye ubora wa kiwango cha juu.

"Nimeshaanza pia kujifunza elimu ya biashara na kuboresha lugha ya Kiingereza kwa sababu nimekuwa nikikutana na mapromota wengi wa kimataifa,"alisema.

Diamond alisema anatarajia kuingia mkataba na Kampuni ya Fuse ya Uingereza, ambayo imewahi kufanyakazi na wasanii wengi maarufu wa Afrika Magharibi na Fally Ipupa wa DRC.

"Unajua muziki mzuri pekee hautoshi kukufanya uwe mwanamuziki wa kimataia. Lazima uwe na sura na mtazamo wa kimataifa,"alisema msanii huyo aliyewahi kunyakua tuzo kadhaa za muziki za Kilimanjaro.

Diamond alisema haamini iwapo imani za ushirikina zinaweza kumsaidia msanii kupata mafanikio. Alisema anawafahamu watoto wengi wa waganga wa kienyeji, lakini hakuna hata mmoja aliyepata mafanikio makubwa kimaisha.

Alisema mafanikio katika maisha yanapatikana kutokana na mipango ya Mungu na kuongeza kuwa, aliyeandikiwa kupata, hakuna anayeweza kuzuia riziki yake.

"Sijawahi kwenda kwa mganga wa kienyeji hata siku moja katika maisha yangu. Utaratibu wangu ni kuamka usiku na kufanya ibada, nikimuomba Mungu anisaidie. Namuomba sana Mungu,"alisema.

Diamond alisema katika uendeshaji wake wa kazi za muziki, amekuwa akisaidiwa na watu 12, kila mmoja akiwa na kazi yake. Alisema miongoni mwa watu hao, wamo madansa wanne, mtaalamu wa mavazi, wapiga picha wawili, mlinzi na msaidizi wake wa karibu.

Alisema hawezi kukaa na mtu, ambaye hawezi kumsaidia kimuziki na kuongeza kuwa, wapo ndugu zake, ambao wamekuwa wakipenda kusafiri naye, lakini anawakatalia kwa sababu hawawezi kuwa na manufaa kwake.

Diamond alisema miongoni mwa mambo anayotarajia kuyafanya ili kuhakikisha maisha yake hayatetereki ni pamoja na kuwekeza katika ardhi.

"Mimi ni mwoga wa maisha. Nimepitia katika mazingira magumu. Hata niwe na pesa kiasi gani, siwezi kusahau maisha niliyopitia. Wakati mwingine huwa napenda kwenda hoteli ya Slipway, nakaa baharini na kukumbuka nilikotoka, huwa nalia sana,"alisema.

"Ndio sababu nimeamua kuwekeza katika ardhi. Ninamiliki nyumba nyingi. Si sahihi kuwa na fedha nyingi benki, lakini hazizalishi. Nimeshindwa kufanya biashara kubwa kutokana na kukosa wasimamizi,"aliongeza.

Diamond alisema kamwe hapendi kutumia pesa zake kuwahonga wanawake. Alisema amekuwa akifanya hivyo kwa sababu maalumu na kwa jambo la msingi.

Msanii huyo alisema thamani ya mali alizonazo kwa sasa, ni zaidi ya shilingi bilioni moja na ushehe na kutamba kuwa, tangu 2011, haijawahi kutokea akaunti yake kupungua sh. milioni 100.

Licha ya kutunga nyimbo nyingi, Diamond alisema anavutiwa zaidi na 'Binadamu', 'Ukimuona', 'Nenda kamwambie', 'Nitarejea' na 'Lala salama'.

Alisema wimbo wa 'Ukimuona' aliutuinga maalumu kwa ajili ya mpenzi wake wa zamani, Wema Sepetu wakati wimbo wa Mawazo aliutunga kwa ajili ya mpenzi wake mwingine wa zamani, Jacqueline Wolper.

Alimtaja mwanamke mwingine aliyewahi kumtungia nyimbo kuwa ni mpenzi wake wa kwanza, anayejulikana kwa jina la Sara. Alizitaja nyimbo hizo kuwa ni Mbagala na Nenda kamwambie.

"Sara ndiye mwanamke wangu wa kwanza. Alinipenda japokuwa sikuwa na kitu. Lakini huko mbele alinieleza wazi kwamba, hawezi kuwa na mwanaume asiyekuwa na maslahi kwake. Nilipatwa na uchungu sana,"alisema.

Diamond alisema anapenda kutunga nyimbo zake kwa kufuata mashairi ya muziki wa taarab, ikiwa ni pamoja na kutumia maneno ya kiswahili yenye mvuto.

Je, ni kwa nini Diamond aligoma kupokea fedha alizotuzwa na Wema wakati wa onyesho lake lililofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City?

"Wakati ule nilikuwa bado nina hasira sana baada ya kugombana na Wema. Alinilaghai kimapenzi. Nilikuwa na hasira sana. Nilijifanya kama simuoni,"alisema.

Hata hivyo, Diamond alikiri kuwa hajawahi kutokea kumpenda mwanamke kama ilivyokuwa kwa Wema. Alisema hata mama yake na rafiki zake wanautambua ukweli huo.

Aliitaja skendo iliyowahi kuripotiwa na vyombo vya habari na kuumiza moyo wake kuwa ni ile iliyomuhusisha mama yake na meneja wake, Papaa Misifa kwamba wana uhusiano wa kimapenzi.

"Habari hiyo iliniumiza sana. Ni bora mtu acheze na kitu chochote kuhusu mimi,lakini siyo mama yangu. Naweza kufanya lolote,"alisema.

"Ni bora tucheze ulingoni wenyewe kwa wenyewe, usimchezee mama yangu. Baada ya Mungu na yeye siogopi kitu kingine chochote na ninaweza kufanya lolote baya. Sintaogopa kwenda jela iwapo itatokea mtu anamuhusisha mama yangu na mambo mabaya,"aliongeza.

No comments:

Post a Comment