KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, June 5, 2013

BRANDTS AMCHIMBIA MKWARA NGASA

KOCHA Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts amebariki kuondoka kwa mshambuliaji Hamisi Kiiza kutoka Uganda, lakini amemchimbia mkwara mshambuliaji mpya, Mrisho Ngasa.

Brandts amesema hana tatizo kuhusu uamuzi wa Kiiza kuondoka Yanga baada ya kushindwa kuelewana na uongozi kuhusu mkataba mpya kwa vile lengo lake lilikuwa ni kutaka kuongezewa pesa.

Kocha huyo alisema hayo juzi usiku baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dar es Salaam akitokea Ubelgiji alikokwenda kwa mapumziko.

"Acha aende, kama anataka fedha nyingi kuliko wenzake, aendetu. Viongozi watafute mchezaji mwingine,"alisema kocha huyo aliyepokewa na Meneja wa Yanga, Hafidh.

Akimzungumzia Ngasa, kocha huyo alisema ni mchezaji mzuri na anaufahamu vyema uwezo wake, lakini amemtahadharisha kwa kusema kuwa, kupangwa kwake kutazingatia uwezo wake mazoezini.

“Inabidi anihakikishie uwezo wake kuanzia mazoezini ili nimpange, vinginevyo nitakuwa nakaa naye benchi,”alisema.

Brandts alisisitiza kuwa, sera yake ni kuangalia uwezo wa kila mchezaji mazoezini na hatampanga mtu kwa sababu ya jina lake.

Mbelgiji huyo alisema lengo lake ni kuiona Yanga ikicheza kwa kasi zaidi msimu ujao, lakini alikiri kuwa, tatizo kubwa linalowakabili kwa sasa ni kukosa uwanja mzuri wa mazoezi.

Kocha huyo alieleza kusikitishwa kwake na mahudhurio hafifu ya wachezaji katika mazoezi yaliyoanza wiki iliyopita kwenye uwanja wa shule ya sekondari ya Loyola iliyopo Mabibo, Dar es Salaam.

Alisema iwapo hali hiyo itaendelea, mashabiki wa Yanga wasitarajie timu hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Kombe la Kagame yanayotarajiwa kuanza Juni 18 mwaka huu nchini Sudan.

“Nimeambiwa wachezaji saba tu wa kikosi cha kwanza ndio wanafika mazoezini, wengine wote ni wa kikosi cha pili. Sasa hii si nzuri, lakini kwa sasa siwezi kulizungumzia sana hili, hadi nitakapokutana na uongozi. Nahitaji nidhamu katika timu ili kutimiza malengo na kuwafurahisha mashabiki wetu,”alisema.

Brandts alisema wakati anaondoka nchini, aliuagiza uongozi kusajili wachezaji wapya wazuri katika kila idara ili kuongeza ushindani wa kuwania namba katika kikosi cha kwanza.

No comments:

Post a Comment