KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 14, 2013

LIGI YA MABINGWA YA MIKOA KUANZA KESHO


MECHI za kwanza za hatua ya tatu ya michuano ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) kuwania nafasi tatu za kupanda Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu ujao, zinatarajiwa kuchezwa keshokutwa.

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema jana kuwa, mechi za marudiano zinatarajiwa kuchezwa Juni 19 mwaka huu.

Wambura alisema Kamati ya Mashindano ya TFF ilikutana juzi mjini Dar es Salaam kwa ajili ya kupitia ripoti za michezo iliyopita na kufanya uamuzi mbalimbali, ikiwemo mechi ya marudiano kati ya Mpwapwa Stars na Machava FC, ambayo haikuchezwa.

Ofisa huyo wa TFF alisema, Machava FC, ambayo ilishinda mechi ya kwanza iliyochezwa mjini Moshi kwa mabao 2-0, inaendelea katika hatua ya tatu kwa vile haikuhusika katika kukwamisha mchezo wa marudiano uliopangwa kuchezwa Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Wambura alisema Chama cha Soka cha Dodoma (DOREFA) kiliuhamishia mchezo huo kwenye Uwanja wa Mgambo mjini Mpwapwa kinyume na maelekezo ya Kamati ya Mashindano ya TFF.

"Kamati katika kikao chake cha awali iliekeleza kuwa mechi zote za RCL zitachezwa makao makuu ya mikoa, isipokuwa kwa Morogoro ambapo timu ya Techfort FC iliruhusiwa kutumia Uwanja wa CCM Mkamba mjini Ifakara,"alisema.

Wambura alizitaja timu nane zilizofuzu kucheza raundi hiyo kuwa ni Friends Rangers ya Dar es Salaam, Kariakoo ya Lindi, Katavi Warriors ya Katavi, Kimondo SC ya Mbeya, Machava ya Kilimanjaro, Njombe Mji ya Njombe, Polisi Jamii ya Mara na Stand United FC ya Shinyanga.

Wakati timu nyingine zimefuzu kwa kushinda mechi zao za raundi ya pili, Njombe Mji imeingia hatua hiyo kwa kuwa timu yenye uwiano mdogo wa kufungwa (best looser) katika hatua ya pili.

Kwa mujibu wa ratiba, katika mechi za hatua hiyo, Kariakoo itamenyana na Friends Rangers, Machava FC na Stand United FC, Polisi Jamii na Katavi Warriors, Kimondo SC na Njombe Mji. Timu zilizoanza kutajwa ndizo zinazoanzia nyumbani.

Wambura alisema kamati ya mashindano imeagiza kamishna wa mechi ya marudiano kati ya Mpwapwa Stars na Machava FC, Mwijage Rugakingira wa Tanga, ambaye alikwenda uwanja wa Mgambo badala ya Uwanja wa Jamhuri kinyume na maelekezo ya TFF, aondolewe kwenye orodha ya makamishna.

Aliongeza kuwa, waamuzi wa mechi hiyo ambao nao walikwenda Mpwapwa badala ya Dodoma Mjini, wamepelekwa mbele ya Kamati ya Waamuzi ya TFF kwa ajili ya kuchukuliwa hatua kutokana na tukio hilo.

"Kamati ya Mashindano imekumbusha kuwa RCL ni mashindano yanayosimamiwa na TFF, hivyo maelekezo yoyote kuhusiana na mashindano hayo, yatatoka TFF na si mahali pengine popote. Msimamizi wa kituo hana mamlaka ya kubadili uwanja,"alisema.

Wambura alisema hatua ya nne ya RCL itachezwa kati ya Juni 23 na 23 mwaka huu wakati mechi za marudiano zitachezwa kati ya Juni 29 na 30 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment