KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 14, 2013

AZAM YAMTOSA KASEJA



UONGOZI wa klabu ya Azam umesema hauna mpango wa kumsajili kipa namba moja wa klabu ya Simba na timu ya Taifa, Taifa Stars, Juma Kaseja.

Meneja Msaidizi wa Azam, Jemedari Saidi alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, kikosi chao kwa sasa kimekamilika katika idara zote.

Jemedari alisema kikosi cha Azam kinao makipa watatu walio kwenye kiwango cha juu kisoka, akiwemo kipa namba moja Mwadini Ally na Aishi Manula.

"Tumekuwa tukisia taarifa kupitia kwenye vyombo vya habari kwamba Azam ina mpango wa kumsajili Kaseja kwa ajili ya msimu ujao, lakini msimamo wetu ni kwamba hatutasajili mchezaji yeyote kutoka klabu za ligi kuu,"alisema.

"Uamuzi uliofikiwa na benchi la ufundi ni kwamba, tutawapandisha vijana wetu kutoka kikosi cha pili na tayari tumeshafanya hivyo. Pia hatuna mpango wa kusajili wachezaji wapya kutoka nje ya nchi,"aliongeza.

Kumekuwa na taarifa zenye utata kuhusu hatma ya Kaseja kwenye kikosi cha Simba baada ya mkataba wake kumalizika mwezi uliopita.

Viongozi wa klabu hiyo kongwe nchini wamekuwa wakivutana kuhusu kipa huyo, baadhi yao wakitaka aongezwe mkataba mpya na wengine wakitaka aachwe.

Alipoulizwa kuhusu hatma ya mchezaji huyo, Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itang'are alisema jana kuwa, itajulikana hivi karibuni.

"Kwa sasa sina la kusema, lakini wakati utakapofika, kila kitu kitakuwa wazi,"alisema.

No comments:

Post a Comment