KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, September 20, 2015

YANGA HII WEEE ACHA TU, YAIBAMIZA JKT RUVU 4-1


YANGA SC imetoa onyo kwa mahasimu wao, Simba SC kuelelea mchezo ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya kuwatandika JKT Ruvu mabao 4-1 jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo wa tatu mfululizo unaifanya Yanga SC itimize pointi tisa na kujiimarisha kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inayoonyeshwa moja kwa moja na Azam TV.
Hadi mapumziko, Yanga SC walikuwa mbele kwa bao 1-0 lililofungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Zimbabwe, Donald Ngoma dakika ya 30 akimalizia pasi fupi ya Amissi Tambwe baada ya kazi nzuri ya kiungo wa kulia Deus Kaseke.
Yanga SC ilitawala mchezo kipindi cha kwanza, lakini haikuweza kutengeneza nafasi nyingi za kufunga mabao, wakati JKT walicheza kwa kujihami zaidi kipindi hicho.
Kipindi cha pili, Yanga SC walirudi na kasi ya kusaka mabao zaidi na iliwachukua dakika tatu tu kupata bao la pili, lililofungwa na Mrundi, Amissi Tambwe aliyemalizia krosi ya Kaseke.
JKT wakafanikiwa kupata bao la kufutia machozi dakika ya 49, kupitia kwa beki na Nahodha wake, Geogre Minja aliyetumia mwanya wa wachezaji wa Yanga SC kuzubaa baada ya kupata bao la pili.
Mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara misimu miwili iliyopita, Amissi Tambwe akaifungia Yanga SC bao la tatu dakika ya 62 kwa kichwa akimalizia krosi ya Simon Msuva. 
Kiungo Mzimbabwe, Thabani Kamusoko akahitimisha sherehe za mabao Yanga SC kwa kufunga bao la nne, dakika ya 87 kwa shuti la nje ya boksi baada ya kukutana na mpira uliookolewa na Michael Aidan kufuatia mpira wa adhabu uliopigwa na Mbuyu Twite baada ya Msuva kuangushwa.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo jioni ya leo, Stand United imeshinda 2-0 dhidi ya African Sports ya Tanga Uwanja wa Kambarage, Shinyanga mabao yote yakifungwa na Elias Maguri, wakati Uwanja wa Mkwakwani, Tanga bao pekee Fully Maganga limeipa Mgambo Shooting ushindi wa 1-0 dhidi ya Majimaji FC na Uwanja wa Sokoine, Mbeya Prisons imeshinda 1-0 dhidi ya Mbeya City bao pekee la Jumanne Elfadhil.
Ligi hiyo itaendelea kesho kwa mechi nne, Mwadui FC na Azam FC Uwanja wa Mwadui Complex, Mtibwa Sugar na Ndanda FC Uwanja wa Manungu, Turiani, Morogoro, Simba SC na Kagera Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na Coastal Union na Toto Africans Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Mwinyi Hajji, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Thabani Kamusoko, Simon Msuva, Haruna Niyonzima/Salum Telela dk78, Amksi tambwe, Donald Ngoma na Deus Kaseke/Godfrey Mwashiuya dk61.
JKT Ruvu; Tony Kavishe, Michael Aidan, Napho Zuberi, Martin Kazila, Ramadhani Madenge, George Minja, Ismail Aziz/Abdulrahman Mussa dk57, Nashon Naftali, Samule Kamuntu/Gaudence Mwaikimba dk57, Saad Kipanga/Emmanuel Pius dk77 na Mussa Juma.
IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BIN ZUBEIRY

No comments:

Post a Comment