KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, September 9, 2015

'MAPROO' WAPIGWA 'STOP' LIGI KUU




NA VICTOR MKUMBO
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limesema kuwa ni marufuku kwa klabu za ligi kuu kuwachezesha wachezaji wa kimataifa katika michuano ya ligi kuu msimu huu iwapo hazitawalipia ada ya Dola za Kimarekani 2,000 (sawa na sh. milioni 4.6).
Katika mkutano wa Kamati ya Utendaji uliofanyika mwaka huu, Zanzibar, kamati ilikubaliana kuwa kila mchezaji ambaye atasajiliwa na klabu ya ligi kuu msimu huu, atalipiwa ada ya Dola 2,000 kabla ya kuanza kwa ligi hiyo.
Hata hivyo, baadhi ya klabu zimeshatangaza kugomea kulipa ada hiyo kwa madai kuwa uamuzi huo umechukuliwa kwa kushtukiza.
Kamati ya Utendaji ya TFF ilifikia makubaliano hayo ili wachezaji wa kimataifa waliosajiliwa Tanzania, waweze kuchangia fedha hizo kwa ajili ya maendeleo ya soka ya wanawake na vijana.
Akizungumza Dar es Salaam, jana, Ofisa Habari wa TFF, Baraka Kizuguto, alisema wameamua kuzikumbusha klabu zote zilizosajili wachezaji wa kigeni ili kuwalipia ada hiyo.
Alisema katika ligi kuu msimu huu, wapo wachezaji 27 wa kigeni, waliosajiliwa na timu mbalimbali, zikiwemo Simba, Yanga  na Azam. Klabu hizo zimesajili wachezaji saba kila moja.
Kizuguto alisema  wachezaji wengine wa kigeni wamesajiliwa katika timu za Mbeya City, Stand United, African Sports na Coastal Union.
“Tunazikumbusha klabu za Ligi Kuu Bara zilizosajili wachezaji kutoka nje ya nchi, kuwalipia ada ya Dola 2,000 kwa kila mchezaji kabla ya ligi kuanza,” alisema.
Aliongeza kuwa klabu itakayolipia idadi ndogo ya wachezaji au wote saba, ndio itakaowatumia kwa  msimu huu na si vinginevyo.
Ofisa huyo alisema wanatarajia kutoa majina ya timu na orodha ya wachezaji waliolipiwa ada baada ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Bara, Jumamosi wiki hii.

No comments:

Post a Comment