KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, September 22, 2015

MALINZI AFUNGA KOZI YA MAKOCHA, AWAPA ANGALIZO




RAIS wa Shirikisho la soka nchini (TFF), Jamal Malinzi, amefunga kozi ya wiki mbili ya makocha lesseni C inayotambuliwa na Shirikisho la soka barani Afrika (CAF) na kuwataka wahitimu hao kufanyia kazi mafunzo waliyoyapata.

Akizungumza kwenye hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo, Malinzi amesema kuwa anasikitika kuona makocha wanapata mafunzo kama hayo lakini wanaenda kuweka vyeti vyao ‘makabatini’ na kuacha kufanyia kazi walichojifunza.

“Hiki mlichokipata kwenye mafunzo haya mnatakiwa muende mkafanyie kazi kwa kutafuta timu za kufundisha na baada ya mwaka mmoja ni vizuri mkajiendeleza zaidi ya hapa,” alisema Malinzi

Amesema kuwa Shirikisho lake limepanga kuhakikisha baada ya muda litafuta utaratibu wa makocha wenye lesseni C kuwa kwenye benchi la ufundi la timu za daraja la kwanza na kuwa wasaidizi kwenye benchi la ufundi la timu za ligi kuu.

“Kwa sasa hivi makocha wa ligi kuu wanatakiwa kuwa na leseni ya daraja B na wasaidizi angalau leseni daraja C, ila kuanzia msimu wa 2017-2018 mambo yatabadilika na lessen I C aizataruhusiwa kwenye mabenchi ya ufunzi kwa timu za ligi kuu, mambo yataendelea hivyo mpaka mwisho tutakuwa na leseni za daraja A,” alisema Malinzi.

Aidha, aliwataka wahitimu hao ambao wengi wao wanatoka kwenye klabu za daraja la kwanza na wengine wakiwa makocha wasaidizi kwenye klabu za ligi kuu, kuhakikisha wanatumia ujuzi walioupata kwenye mafunzo hayo kuzisaidia timu zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha soka mkoa wa Dar es Salaam, Almas Kasongo, ameishukuru TFF kwa jitihada za kuendeleza mchezo wa soka nchini na kuelelezea changamoto wanazokutana nazo katika kuandaa kozi kama hizo kwa vyama vya soka vya mikoa nchini.

“Sisi DRFA tumefanikiwa kuendesha kozi hii kwa sababu ya uwepo wa timu za Simba, Yanga na Azam kwenye ligi kuu ambazo ni sehemu ya mapato kwa chama chetu, ila kwa vyama vingine hali inakuwa ngumu kuandaa na kuendesha mafunzo kama hayo,” alisema Kasongo.

Kozi hiyo ya wiki mbili ilikuwa ikifanyika kwenye ukumbi wa TFF na kuendeshwa na mkufunzi anayetambulika na CAF, Salum Madadi ambaye pia ni Mkurugenzi wa ufundi wa TFF.

No comments:

Post a Comment