KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, September 13, 2015

NGOMA, MSUVA WAIUA COASTAL UNION




NA AMINA ATHUMAN
MABAO mawili yaliyofungwa na Simon Msuva na Donald Ngoma yameiwezesha Yanga kuibuka na ushindi katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Coastal Union.
Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga iliandika bao lake la kwanza dakika ya saba kupitia kwa Msuva aliyeachia shuti kali akiunganisha pasi ya Kelvin Yondan.
Bao la pili lilipatikana dakika ya 42 baada ya Ngoma kuunganisha mpira uliorudi uwanjani baada ya kipa wa Coastal Union kupangua mpira wa krosi iliyochongwa na Msuva.
Katika mchezo huo, Yanga ilianza mchezo kwa kasi na kushambulia lango la wapinzani wao kama nyuki ikitafuta mabao ya kufunga.
Dakika ya 12 Coastal Union ilibadilisha mfumo wa uchezaji na wachezaji wake kurudi nyuma kwa ajili ya kuzuia mashambulizi.
Hali hiyo ilisaidia kupunguza kasi ya Yanga lakini dakika ya 18 Niyonzima alibaki na kipa Sebwato Nicholas, lakini shuti alilopiga lilitoka pembeni kidogo ya goli.
Coastal Union ilijibu shambulizi hilo dakika ya 23 ambalo halikuzaa matunda kabla ya kufanya mabadiliko na kumtoa Adeyum Ahmed na kuingia Twaha Ibrahim
Mabadiliko hayo yaliamsha ari ya wachezaji wa Coastal Union ambapo dakika ya 29 Ali Ahmed alipata nafasi ya kufunga na kuachia shuti kali lililopaa mita chache na kutoka nje.
Coastal Union ilipata nafasi nyingine dakika ya 76 kupitia kwa Patrick Protas baada ya kubaki na kipa lakini mpira aliopiga ulitoka pembeni kidogo ya goli.
Timu zote ziliendelea kushambuliana kwa zamu lakini hadi dakika 90 zinamalizika Yanga ndiyo iliyoondoka uwanjani na kicheko baada ya kupata pointi tatu.

Ali Mustapha, Mbuyu Twite, Haji Mwinyi, Nadir Haroub, Kelvin Yondan, Thaban Kamusoko, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amis Tambwe/Malimi Busungu, Donald Ngoma na Godfrey Mwashiuya/Deus Kaseke.
Coastal Union:Sebwato Nicholas, Hamad Juma, Yasin Mustapha, Ernest Joseph, Tumba Sued, Said Jeilan/Patrick Protas , Ali Ahmed, Yousoufa Sabo, Nasoro Kapama, Godfrey Wambura na Adeyum Ahmed.

No comments:

Post a Comment