KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, September 28, 2015

DIAMOND APASUA JIPU SAKATA LA MWANAWE



NA NASRA KITANA

WATANZANIA wengi walikuwa wanaisubiri siku maalumu ambayo staa wa muziki nchini na Afrika, Nassib Abdul 'Diamond Platinum' ataweka hadharani sura ya mtoto wake.

Pia wapenzi wa burudani walikuwa na shauku ya kuona sura ya mtoto huyo ambaye alizua gumzo tangu mama yake Zarina Hassan 'Zari The Boss Lady' akiwa mjamzito.

Shauku hiyo iliongezwa kasi baada ya kuenea tetesi kuwa Diamond alibambikiwa ujauzito huo lakini yeye hakujali na aliendelea na maandalizi ya kumpokea mwanawe mtarajiwa.

Baada ya mtoto wa kike kuzaliwa, yaliibuka maneno lukuki kuwa si mwanawe na baadhi ya wadau walitaka apimwe vinasaba (DNA) ili kupata ukweli.

Septemba 20, mwaka huu mtoto wa mastaa hao alipewa jina la Latiffah 'Tiffah', alitimiza siku 40 na nyota hao waliamua kufanya sherehe kamambe ya kumkaribisha rasmi duniani.

Sherehe hiyo iliyojumuisha nyota mbalimbali wakiwemo wa filamu, ilifanyika nyumbani kwake Madale-Tegeta, Dar es Salaam.

Diamond na Zari wamezishawishi baadhi ya kampuni kubwa za biashara kuingia mkataba wa malipo kutumia jina na picha za Tiffah kibiashara.

Tayari kinda huyo ni balozi wa maduka ya nguo za watoto Dar es salaam na pia picha yake ya kwanza ilioneshwa hadharani ikiambatana na udhamini wa benki ya NMB.

Diamond anasema mtoto wake Tiffah ni 'photocopy' ya sura yake na anashukuru mtoto huyo amefuata rangi ya urembo wa mama yake.

Anasema anashukuru Mungu kupata mtoto ambaye ilikuwa ndoto ambapo ameahidi kumtunza na kumpa malezi bora katika maadili ya Afrika.

"Kwanza nimefurahi kwa sababu mtoto ni kopi yangu kabisa huwezi kukataa na wale waliokuwa wanadai kwamba nimesingiziwa nadhani wamethibitisha hilo baada ya kuona piacha zake,"alisema Diamond.

“Unajua mtoto kama si wako ni rahisi tu kujua. Na unajua mzazi anakuwa mtu wa kwanza kugundua kama mtoto si wako.

Kuhusu kauli zinazoenezwa kuwa mtoto huyo si wake, Diamond, anasema wabaya wake wamekuwa wakimfuatilia muda mrefu lakini wameshindwa.

“Mimi nasema jamani nyinyi mnadai mna hela, matajiri mmeshamwacha mwanamke mbona mmekuwa mnafuatilia.Fanyeni shughuli zingine, tafuteni wanawake wengine wazuri zaidi yake mfanye vitu vingine," anasema Diamond.

Mwimbaji huyo anasema matarajio yao ni kupata mtoto wa pili ambaye atazaa na Zari baada ya mtoto wao Tiffah 'kuchangamka'.

Akizungumzia mustakabali wa maisha yao, Diamond, anasema wanatarajia kufunga ndoa hivi karibuni kwa sababu hakuna kikwazo baina yao.

No comments:

Post a Comment