KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, September 8, 2016

SIMBA, AZAM ZATAKATA LIGI KUU, AZAM YABANWA

BAO lililofungwa na mshambuliaji, Laudit Mavugo katika kipindi cha pili jana liliiwezesha Simba kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ruvu Shooting katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Mavugo, mshambuliaji wa kimataifa kutoka Burundi, alifunga bao hilo dakika tatu baada ya kuanza kwa kipindi cha pili, baada ya kumalizia pasi maridhawa kutoka kwa Ibrahim Ajib.

Katika mechi hiyo ya kwanza ya ligi kuchezwa kwenye uwanja huo, baada ya kukarabatiwa na kukabidhiwa kwa serikali, Ruvu Shooting ilikuwa ya kwanza kupata bao.

Bao hilo lilifungwa na Abdulraman Mussa dakika ya saba, baada ya mabeki wa Simba kuzembea kuokoa mpira uliopigwa na Fully Maganga.

Simba ilisawazisha dakika ya 11 kwa bao lililofungwa na Ajib, akimalizia krosi kutoka kwa beki wa kushoto, Mohamed Hussein 'Tshabalala'. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa sare ya bao 1-1.

Katika mechi hiyo ya kusisimua, Simba ingeweza kutoka uwanjani na ushindi mkubwa wa mabao, lakini umaliziaji mbovu wa washambuliaji wake, Ajib, Shiza Kichuya na  Mavugo ulikuwa kikwazo.

Mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Yanga walishindwa kutambe mbele ya Ndanda FC baada ya kulazimishwa kutoka nayo suluhu katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.

Wakati huo huo, Azam FC jana iling'ara ugenini baada ya kuichapa Prisons bao 1-0 kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Bao pekee na la ushindi la Azam lilipachikwa wavuni na Kipre Balou katika kipindi cha pili.

No comments:

Post a Comment