KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, September 18, 2016

NI KUFA NA KUPONA KWA KILIMANJARO QUEENS LEO, INACHEZA NUSU FAINALI DHIDI YA UGANDA



TIMU ya taifa ya Tanzania Bara ya wanawake, Kilimanjaro Queens leo inashuka kwenye Uwanja wa Ufundi, Njeru mjini Jinja, Uganda kumenyana na wenyeji, Korongo Jike katika Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge.
Kocha wa Kilimanjaro Queens, Sebastian Nkoma amesema kwamba hakutaka vijana wake kutumia nguvu nyingi katika mchezo wa mwisho wa Kundi B, ili kuzitunza kwa ajili ya Nusu Fainali.
“Nilijua tutacheza na ama Kenya au Uganda katika Nusu Fainali, zote ni timu ngumu, kwa hiyo tukacheza kwa maarifa sana mechi yetu na Ethiopia, ili tusijichoshe sana na kukwepa pia wachezaji kupata maumivu. Tumefanikiwa na sasa tunaelekeza nguvu zetu katika Nusu Fainali,”alisema Nkoma. 
Tanzania imeongoza Kundi B baada ya kushinda kura ya sarafu juzi kufuatia sare ya 0-0 na Ethiopia hivyo kufungana nayo kwa pointi na wasatani wa mabao kileleni, wakati Uganda imeshika nafasi ya pili Kundi A nyuma ya Kenya.
Kwa matokeo hayo, mbali na Kilimanjaro Queens kumenyana na wenyeji Uganda – Nusu Fainali ya itazikutanisha Kenya na Ethiopia.
Kilimanjaro Queens ilianza vizuri michuano hiyo kwa kuibamiza 3-2 Rwanda, mabao yake yakifungwa na Asha Rashid ‘Mwalala’ dakika za 11 na 65 na Stumai Abdallah dakika ya 28, wakati ya wapinzani wao yalifungwa na Ibangarrue Marie na Amina Ally wa Tanzania Bara aliyejifunga.
Fainali ya CECAFA Challenge ya kwanza ya wanawake inatarajiwa kufanyika Septemba 20, ikitanguliwa na mchezo wa kusaka mshindi wa tatu.

No comments:

Post a Comment