KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 11, 2015

KUZIONA STARS, ALGERIA BUKU TANO


Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) limetangaza viingilio vya mchezo wa Jumamosi kati ya Tanzania dhidi ya Algeria utakaochezwa katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam bei ya chini kuwa ni shilingi elfu tano (5,000) tu.

Tiketi za mchezo huo zitaanzwa kuuzwa siku ya ijumaa katika vituo mbalimbali vinavyotumiwa na TFF kuuzia tiketi, ambapo kiingilio kingine kitakua ni elfu kumi (10,000) kwa viti vya VIP B & C, huku kiingilio cha elfu tano kikiwa ni kwa viti vya rangi ya Bluu, Kijani na rangi ya Machungwa.

Wakati huo huo kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kinachodhamininiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager, kinatarajiwa kurejea nyumbani kesho Jumatano mchana kwa shirika la ndege la Fastjet tayari kwa maandalizi ya mwisho ya mchezo dhidi ya Algeria siku ya Jumamosi.

Stars iliyoweka kambi nchini Afrika Kusini imekua ikifanya mazoezi kila siku katika uwanja wa Edenvale, ambapo mpaka sasa wachezaji wote wapo katika hali nzuri hakuna majeruhi na kila mmoja yupo tayari kwa mchezo wa Jumamosi.

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Mkwasa amesema vijana wake wapo vizuri kifaya, kifikra na morali ni ya hali juu “wachezaji wamekua wakifanya mazoezi kwa nguvu na kuonyesha umakini mkubwa” alisema Mkwasa.

Aidha, Mkwasa amewaomba watanzania na wadau wote wa mpira wa miguu nchini kujitokeza kwa wingi kuwapa sapoti ya kuwashangilia vijana katika mchezo dhidi ya Algeria Jumamosi, kwani kutawafanya wachezaji kujisikia wapo nyumbani na kucheza kwa nguvu zaidi.

Wachezaji wa kimataifa wa Tanzania Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu walioshinda kombe la Ligi ya Mabingwa mwishoni mwa wiki na klabu yao ya TP Mazembe wanatarajiwa kuungana na wenzao kambini kesho jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment