KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, May 11, 2015

ABDALLA KIBADENI: VIONGOZI WENGI WA SOKA BOMU




KOCHA maarufu wa soka nchini, Abdalla ‘King’ Kibadeni, ameamua kuweka mambo hadharani kwa kusema kuwa viongozi wengi wa sasa wa mchezo huo ‘bomu’.
Kibadeni, ambaye alipewa jina la King miaka ya 1970, alipokuwa akiicheza Simba, akifananishwa na Pele wa Brazil, amesema viongozi wengi wa soka nchini hawana mapenzi ya dhati na klabu zao na wameweka mbele zaidi maslahi yao binafsi.
Mbaya zaidi, Kibadeni amesema baadhi ya viongozi wa klabu hawapendani, hawana uzalendo na wamekuwa wakiwadhulumu wachezaji haki zao za msingi.
Mshambuliaji huyo nyota wa zamani wa Simba na timu ya Taifa, Taifa Stars, alisema hayo mjini Dar es Salaam hivi karibuni, alipokuwa akizungumzia maendeleo ya mchezo huo nchini na mustakabali wake kisoka.
Kibadeni, ambaye alipewa hadhi ya ‘Chifu Mputa’, alipokuwa akiifundisha Majimaji ya Songea,amesema kushindwa kufanya vizuri kwa timu za Tanzania katika michuano ya kimataifa, kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na uzembe wa viongozi.
Amesema katika miaka ya nyuma, timu za Tanzania zilikuwa zikifanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa kutokana na viongozi wake kuwa makini katika maandalizi na kuwahudumia wachezaji.
“Zamani haikuwa ajabu kwa Simba, Yanga, Pan African na Taifa Stars kuzifunga timu za Afrika Magharibi. Hawakuwa wakitusumbua,”alisema.
Amesema ajira ya ukocha kwa klabu za Tanzania haina heshima kutokana na kutimuliwa bila sababu za msingi na pia baadhi ya viongozi kuingilia kazi zao, ikiwa ni pamoja na kupanga wachezaji katika mechi muhimu.
“Viongozi kuingilia kazi za kocha ni jambo la kawaida. Unaweza ukaletewa memo siku ya mechi ikikuelekeza timu inayopaswa kucheza siku hiyo na ukikataa kufuata maelekezo, unajiweka kwenye matatizo,”amesema kocha huyo aliyewahi kuzifundisha timu za Majimaji, Moro United, Manyema, Ashanti na Simba.
“Wakati mwingine unaweza kupigiwa simu siku ya mechi, ukaambiwa fulani usimchezeshe, ameonekana mahali fulani akichukua pesa, lakini ukimuuliza iwapo ana ushahidi, hana. Sasa fikiri umemfundisha mchezaji wiki nzima kwa ajili ya maandalizi ya mechi, halafu unaambiwa usimchezeshe,”aliongeza.
Kocha huyo amesema yeye na Julio (Jamhuri Kihwelo), walitimuliwa Simba mwaka jana bila sababu za msingi na kwamba kitendo hicho kiliwahuzunisha.
Amesema kumdhulumu mtu haki zake ni dhambi na pale anapohuzunika, dua yake hupokelewa na Mungu.
Kwa mujibu wa Kibadeni, kufundisha timu ndogo kuna changamoto nyingi, ikiwa ni pamoja na malipo kidogo, lakini kocha anakuwa huru katika kufanyakazi yake.
“Lakini ukifundisha timu kubwa, kama hauko sawasawa, utashindwa. Timu ikifanya vizuri utaonekana wa maana, lakini ikivurunda unashushwa thamani,” amesema.
Ili kocha aweze kulinda hadhi na heshima yake, Kibadeni amesema ni bora kuondoka mapema timu inapofanya vibaya badala ya kusubiri kutimuliwa.
Hata hivyo, Kibadeni amesema wachezaji wamekuwa wakichangia makocha kutimuliwa holela kutokana na kushindwa kucheza kwa kufuata maelekezo wanayopewa.
“Mara nyingi wachezaji wamekuwa wakipaniki mapema katika mechi muhimu na kucheza kivyao, lakini mwisho wa siku, lawama zinamuangukia kocha,”amesema.
Kibadeni amesema katika miaka ya nyuma, makocha walikuwa na heshima kubwa katika klabu za Simba na Yanga, ikiwa ni pamoja na kutumiwa na wanachama kutafuta viongozi bora wakati wa uchaguzi na ushauri wao uliheshimiwa.
Akizungumzia ushiriki wa timu za Tanzania katika michuano ya kimataifa, Kibadeni amesema tatizo kubwa ni maandalizi duni na viongozi kushindwa kuzitumia vyema mechi za nyumbani kupata ushindi.
Amesema ushindi wa nyumbani ni muhimu kwa vile unarahisisha matokeo ya ugenini.
Kwa mujibu wa Kibadeni, waarabu wanapocheza ugenini, hutumia mbinu ya kuchelewesha muda na kucheza kwa kujihami ili kuwachanganya wapinzani wao, lengo lao kubwa likiwa ni kutumia kila mbinu kushinda nyumbani.
Amesema viongozi wa Simba walitumia vyema mbinu hizo katika michuano ya Kombe la CAF mwaka 1993, ambapo walishinda karibu mechi zote za nyumbani na kulazimisha sare ugenini na hatimaye kufuzu kucheza fainali.
Amesema hadi sasa hana hakika ni vipi Simba ilishindwa kutwaa kombe hilo nyumbani baada ya kutoka suluhu na Stella Abidjan ya Ivory Coast ugenini. Katika mechi hiyo ya marudiano iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Simba ilichapwa mabao 2-0.
“Mengi yalisemwa kuhusu mechi hiyo. Wengine walisema ilikuwa ni mbinu ya mfadhili (Azim Dewji) kupita mlango wa nyuma baada ya kushindwa kununua KIA alizoahidi kwa wachezaji.
“Ninachoweza kusema sina hakika. Inawezekana ikawa kweli ama isiwe kweli. Hata mimi nilishindwa kuelewa. Kwao tulitoka sare, tukatawala mchezo, huku tukafungwa!” Alieleza kwa mshangao Kibadeni, ambaye alikuwa kocha msaidizi wa Simba wakati huo, akimsaidia Eshente kutoka Ethiopia.
Kocha huyo amesema timu nyingi zinazoshiriki michuano ya ligi kuu Tanzania Bara, lengo lao kubwa huwa ni kubaki katika ligi hiyo, na si kutwaa ubingwa. Amesema hali hiyo ndiyo inayotoa mwanya kwa Simba, Yanga na sasa Azam kutawala ligi hiyo.
Kibadeni ameelezea kusikitishwa kwake na uamuzi wa Azam kumtimua kocha wake, Joseph Omog kutoka Cameroun, baada ya timu hiyo kutolewa na El-Merreikh ya Sudan katika michuano ya Kombe la Shirikisho mwaka huu.
Amesema uamuzi huo haukuwa wa busara na ulichangia kuifanya Azam ipoteze mwelekeo katika kutetea taji la ligi kuu msimu huu, ambalo limetwaliwa na Yanga.
Akizungumzia mipango yake ya baadaye, Kibadeni amesema ni kukuza vipaji vya vijana kupitia kituo chake cha kuendeleza soka chenye vijana wa umri wa miaka 14 hadi 16.
“Nawakaribisha vijana wa umri huo wenye vipaji waje kwenye kituo changu. Nawaandaa kuwa wachezaji wa timu za taifa za vijana wa umri mbalimbali. Sitarajii kuwauza Simba au Yanga, nitawauza nje,”amesema.
Licha ya kuanzisha na kumiliki kituo hicho, Kibadeni amesema hajawahi kuwaona viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), waliopewa jukumu la kusimamia soka ya vijana, wakimtembelea au kumpatia msaada wowote.
Amesema anakerwa kuona viongozi wa Simba, Yanga na Azam, wakitumia mamilioni ya pesa kusajili wachezaji kutoka nje ya nchi, wakati wapo vijana wengi wenye vipaji, isipokuwa wanatakiwa kuendelezwa.
Licha ya kuwepo kwa vijana wengi wenye vipaji vya kucheza soka nchini, Kibadeni amesema hakuna usimamizi mzuri katika soka ya vijana. Amesema hali hiyo ndiyo inayosababisha hadi sasa kusitokee vijana walioweza kufikia kipaji chake.
“Bado hajatokea mchezaji wa aina yangu hadi sasa, ndio sababu nilipewa majina ya heshima kama vile King, nikifananishwa na Pele na Mputa, nililopewa kama heshima na viongozi wa mkoa wa Ruvuma kutokana na kuinua soka ya mkoa huo,”amesema Kibadeni.





No comments:

Post a Comment