KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, March 15, 2015

YANGA KUDADADEKI! YAWABAMIZA WAZIMBABWE 5-1


YANGA SC imetanguliza mguu mmoja hatua ya 16 Bora Kombe la Shirikisho Afrika kufuatia ushindi wa mabao 5-1 dhidi ya Platinum FC ya Zimbabwe jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ili Yanga isisonge mbele, inabidi ifungwe mabao 4-0 na Platinum katika mchezo wa marudiano wiki ijayo mjini Bulawayo.

Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Djamaladen Aden Abdi, aliyesaidiwa na Hassan Eguech Yacin na Abdallah Mahamoud Iltireh wote wa Djibouti, hadi mapumziko, tayari Yanga SC walikuwa mbele kwa mabao 2-1.

Mabao ya Yanga SC yalifungwa na viungo Salum Abdul Telela ‘Master’ dakika ya 32 na Haruna Niyonzima ‘Fabregas’ dakika ya 43, wakati bao la Platinum lilifungwa na Walter Musoma dakika ya 45.

Kipindi cha pili, Yanga waliongeza makali na kufanikiwa kupata mabao matatu zaidi, ambayo yanawafanya waende Bulawayo kwenye mchezo wa marudiano, wakiwa wana kazi ndogo tu.

Mabao hayo yalifungwa na Amisi Tambwe dakika ya 47 na Mrisho Ngassa mawili dakika ya 55 na 90.
Mshambuliaji Mliberia, Kpah Sherman aliyetokea benchi kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Simon Msuva alimsetia krosi nzuri Ngassa kufunga bao la tano.

Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul/Hassan Dilunga, Oscar Joshua, Kevin Yondan, Mbuyu Twite, Salum Telela, Simon Msuva/Kpah Sherman, Haruna Niyonzima, Amisi Tambwe na Said Juma ‘Kizota’.

Platinum FC; Petros Mhari, Raphael Muduviana, Kelvin Moyo, Gift Bello, Thabit Kamusuko, Wellington Kamudyariwa/Simon Shoko, Wisdom Mtasa/Aaron Katege, Brian Muzondiwa, Obrey Ufiwa/Emmanuel Mandiranga, Walter Musoma na Elvis Moyo.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BINZUBEIRY

No comments:

Post a Comment