KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, July 31, 2014

TAIFA STARS YAENDA AFRIKA KUSINI



Msafara wa watu 27 wa kikosi cha timu ya Taifa (Taifa Stars) kimeondoka nchini juzi saa 10 jioni kwa ndege ya Air Tanzania kwenda Afrika Kusini ambapo kitapiga kambi ya siku mbili kabla ya kuingia Maputo kuikabili Msumbiji (Mambas).

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iliwasili Afrika Kusini saa 9 asubuhi jana kwa ndege ya Fastjet, na baadaye jioni kuunganisha safari ya Afrika Kusini.

Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya pili ya michuano ya Afrika dhidi ya Msumbiji itachezwa Agosti 3 mwaka huu Uwanja wa Taifa uliopo Zimpeto nje kidogo ya Jiji la Maputo.

Msafara huo wa Taifa Stars kwenda Afrika Kusini unajumuisha wachezaji 19 na waliobaki ni maofisa wa Benchi la Ufundi lililo chini ya Kocha Mkuu Mart Nooij kutoka Uholanzi.

Wakati kiungo Mwinyi Kazimoto ametua leo (Julai 29 mwaka huu) nchini kuungana na wenzake, washambuliaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wao wataungana na wenzao kesho (Julai 30 mwaka huu) jijini Johannesburg wakitokea Lubumbashi, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

Wakati huo huo, Serengeti Boys imewasili salama jana (Julai 28 mwaka huu) jijini Johannesburg, Afrika Kusini kwa ajili ya mechi ya michuano ya Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 dhidi Afrika Kusini (Amajimbos).

Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya pili itachezwa Jumamosi, Agosti 2 mwaka huu kwenye Uwanja wa Dobsonville uliopo Soweto kuanzia saa 9 kamili mchana kwa saa za Afrika Kusini.

Timu hizo zilitoka suluhu katika mechi ya kwanza iliyofanyika Julai 18 mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam. Serengeti Boys inahitaji ushindi kwenye mechi hiyo au aina yoyote ya sare ya mabao ili ifuzu kwa raundi ya tatu.

No comments:

Post a Comment