KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, July 27, 2014

SERENGETI BOYS KWENDA AFRIKA KUSINI KESHO



Msafara wa watu 25 wa kikosi cha timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) unaondoka kesho (Julai 28 mwaka huu) kwenda Afrika Kusini kwa ajili ya mechi dhidi ya Afrika Kusini (Amajimbos).

Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya pili itachezwa Jumamosi, Agosti 2 mwaka huu kwenye Uwanja wa Dobsonville uliopo Soweto, Johannesburg kuanzia saa 9 kamili mchana kwa saa za Afrika Kusini.

Timu hizo zilitoka suluhu katika mechi ya kwanza iliyofanyika Julai 18 mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam. Mshindi atacheza raundi ya mwisho ya michuano hiyo ya Afrika na mshindi wa mechi kati ya Misri na Congo Brazzaville.

Fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 zitafanyika mwakani nchini Niger.

Wachezaji wanaounda kikosi cha Serengeti Boys katika msafara huo utakaoondoka saa 2 usiku kwa ndege ya Fastjet ni Abdallah Jumanne Shimba, Abdulrasul Tahil Bitebo, Abutwalibu Hamidu Msheri, Adolf Mtsigwa Bitegeko, Ally Aziz Mnasi, Ally Shaban Mabuyu na Athanas Enemias Mdamu.

Wengine ni Badru Haji Othman, Baraka Yusuph Baraka, Issa Backy Athuman, Juma Ally Yusuph, Kelvin Longnus Faru, Martin Kiggi Luseke, Metacha Boniface Mnata, Mohamed Mussa Abdallah, Omary Ame Omary, Omary Natalis Wayne, Prospal Alloyce Mushin na Seif Said Seif.

Benchi la Ufundi linaongozwa na Kocha Mkuu Hababuu Ally Omary akisaidiwa na Stewart John Hall (Mshauri wa Ufundi), Peter Manyika (Kocha wa makipa), Richard Yomba (Daktari), na Edward Venance (Mtunza vifaa).

Msafara wa timu hiyo itakayorejea nyumbani Agosti 4 mwaka huu unaongozwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Khalid Mohamed Abdallah.

No comments:

Post a Comment