KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, April 2, 2017

SERENGETI BOYS YAITUNGUA TENA BURUNDI



TIMU ya taifa ya vijana ya Tanzania chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys imeendeleza wimbi la ushindi katika mechi zake za kirafiki baada ya  kuifunga Burundi mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.
Ushindi huo ni wa pili mfululizo kwa Serengeti Boys baada ya juzi kuichapa Burundi mabao 3-0 katika mchezo mwingine wa kirafiki.
Katika mechi hiyo, Kocha Bakari Shime, anayefanya kazi chini ya Mshauri wa Ufundi, Kim Poulsen, alifanya mabadiliko makubwa kikosini mwake, akiwapa nafasi zaidi wachezaji ambao hawakucheza mechi ya kwanza.
Wafungaji wa mabao ya Serengeti Boys walikuwa Issa Abdi Makamba dakika ya 36 na Ibrahim Abdallah Ali dakika ya 89.
Serengeti Boys ilitawala sehemu kubwa ya mchezo huo huku wapinzani wao wakicheza rafu nyingi. 
Serengeti Boys imerejea Dar es Salaam, ambako kesho watakuwa na mchezo wa mwisho wa kirafiki dhidi ya Ghana, kabla ya kwenda Morocco kwenye kambi ya mwezi mmoja, kujiandaa na fainali za U-17 Afrika, Mei mwaka huu nchini Gabon.

No comments:

Post a Comment