KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, August 10, 2015

KIHANGA MWENYEKITI FA MOROGORO


Chama cha Mpira wa Miguu mkoa wa Morogoro (MRFA) jana kilifanya uchaguzi wa viongozi wake katika nafasi ya mwenyekiti, makamu mwenyekiti, katibu, mweka hazina, mjumbe wa mkutano mkuu pamoja na wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

Katika uchaguzi huo Paschal Kihanga aliibuka na ushindi katika nafasi ya mwenyekiti, huku Gracian Max Makota  akishinda nafasi ya makamu mwneyekiti, nafasi ya katibu mkuu imechukuliwa na Charles Mwakambaya na katibu msaidizi Jimmy Lengme.

Nafasi ya Mweka Hazina imechukuliwa na Peter Mshigati, Mjumbe wa mkutano mkuu ni Hassan Mamba na mwakilishi wa vilabu ni Ramadhani Wagala, Kamati ya utendaji wamechaguliwa Mrisho Javu, Rajabu Kiwanga na Boniface Kiwale.

TFF inawapongeza viongozi wapya waliochaguliwa kuongoza chama cha soka mkoa wa Morogoro (MRFA) na kuahidi kuendelea kushirikiana nao katika kazi za kila siku za maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

TOTO AFRICAN KUCHAGUANA OKTOBA 2015
Klabu ya Toto African ya Mwanza inatarajiwa kufanya uchaguzi wa kujaza nafasi zilizo wazi katika kamati yake ya utendaji ifikapo tarehe 11 Oktoba 2015. Katika barua yake kwa Katibu Mkuu wa Toto African, Katibu Mkuu wa TFF ameuagiza uongozi wa Toto African kuwasiliana na Kamati yao ya Uchaguzi ili tangazo la uchaguzi litolewe si chini ya siku sitini (60) kabla ya tarehe ya kufanyika uchaguzi.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mvutano katika klabu ya Toto na suala kubwa likiwa ni kuhusu ujazaji wa nafasi zilizo wazi. Awali TFF ilipokea maombi ya wanachama na wadau wa Toto African wakitaka ufanyike uchaguzi ili kumaliza mvutano ndani ya klabu.

TFF ilishauri uchaguzi huo kusubiri klabu kukamilisha mchakato wa usajili.

Vilevile TFF imewataka wadau wote wa klabu hiyo kongwe ya mjini Mwanza kuheshimu uongozi uliopo madarakani kwani ndio unaotambulika na ndio utaendelea kuiongoza Toto African katika kipindi cha kuelekea uchaguzi uchaguzi.

TFF YATUMA SALAM ZA RAMBIRAMBI MALAWI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Jamal Malinzi ametuma salam za rambi rambi kwa Rais wa Chama cha Soka nchini Malawi (FAM), Walter Nyamilandu kufutia kifo cha aliyekua Rais wa chama hicho John Zingale.

John Zangale alifariki dunia baada ya kuugua kwa muda mfupi wiki iliyopita katika hospitali ya  Mlambe iliyopo Blantyre nchini Malawi na kuzikwa mwishoni mwa wiki alikuwa Rais wa FAM mwaka 1998- 2002.

 Katika salam zake kwenda kwa Rais wa FAM, Malinzi amewapa pole familia ya marehemu pamoja na chama cha soka nchini Malawi kwa msiba huo, na kusema TFF kwa niaba ya Watanzania iko pamoja nao katika kipindi hicho cha maombelezo.


No comments:

Post a Comment