KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 22, 2017

YANGA YATANGAZA RASMI KUACHANA NA NIYONZIMA



Taarifa rasmi kutoka klabu ya Yanga ni kwamba, imeamua kuachana na kiungo wake wa kimataifa wa Rwanda Haruna Niyonzima baada ya kushindwa kufikia makubalino kuhusu kuongeza mkataba mpya wa kuendelea kubaki Yanga.

Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa amesema, Yanga imeamua kuachana na Niyonzima baada ya pande hizo mbili kushindwa kufikia makubaliano juu ya kuongeza mkataba mpya ambao ungemfanya Niyonzima aendelee kusalia kwa mabingwa hao wa VPL.

“Tumekuwa na changamoto nyingi haswa katika kipindi hiki cha usajili kuna taarifa mbalimbali zimekuwa zikitoka kuhusiana na mchezaji ambaye alikuwa ni nahodha wetu msaidizi Haruna Niyonzima, ni kweli mkataba wake unakaribia kukamilika na sisi kama viongozi tumefanya jitihada za kukutana naye kujaribu kuongeza mkataba kwa kipindi kijacho kwa sababu bado tulikuwa na nia nae.”

“Tumekuwa tukikaa na kamati pamoja na viongozi kwa kipindi kirefu lakini kumetokea kutoelewa kutokana na matakwa yake yaliyokuwa yamejitokeza kwa hiyo klabu inasema wazi kwamba klabu hakuwa na uwezo wa kile ambacho kilikuwa kinatakiwa na mchezaji kwa hiyo imeshindikana kulingana na hali ya klabu ilivyo.”

“Muda ukifika tutamruhusu na kumtakia kila la heri kule anakokwenda kwa faida yake mwenyewe na familia yake, kweli sisi tulikuwa na nia yake na tulizungumza nae lakini hatukufikia makubaliano  na sisi kwa maslahi ya klabu tumeamua tumruhusu aende kule ambako anaweza kupata maslahi mazuri.”

Kwa mujibu wa Mkwasa, Niyonzima alikuwa akihitaji pesa ndefu ili asaini mkataba mpya kitu ambacho Yanga walishindwa kufikia makubaliano nae na kuamua kumruhusu aende sehemu ambako atapata dau hilo.

“Kwa tamaduni zetu huwa hatusemi ni kiasi gani lakini nafikiri ni kiasi kikubwa siwezi kukitaja kwa umma kwa hiyo kwa maslahi ya klabu tumeona ni bora tufanye utaratibu mwingine kwa sababu tunaweza kufanya usajili mwingine kuliko ambavyo tungeweza kutoa kiasi hicho kwa mtu mmoja.”

Niyonzima amekuwa akihusishwa kujiunga na klabu ya Simba ambayo imekuwa ikimuwinda kwa muda lakini mara kadhaa amekuwa akikanusha taarifa hizo na kudai yeye bado ana mkataba na Yanga.

No comments:

Post a Comment