KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 11, 2017

SARE YA STARS DHIDI YA LESOTHO YAMKERA SAMATTA, ASEMA UWANJA WA AZAM HAUKUPASWA KUTUMIKA KWA MECHI HIYO





NAHODHA wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Mbwana Samatta amesema amekerwa na matokeo ya sare waliyoyapata kutoka kwa Lesotho katika mechi ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika za 2019.

Samatta amesema haikuwapo kwenye akili yake Taifa Stars kupata sare katika mechi hiyo ndio sababu wachezaji wote walipatwa na hasira baada ya mechi hiyo kumalizika.

Katika mechi hiyo iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam, Taifa Stars ilitoka sare ya bao 1-1 na Lesotho, matokeo ambayo yaliwachukiza mashabiki wengi wa soka nchini.

“Kitu ambacho kimewasaidia Lesotho ni uwanja kuwa mdogo. Na kuhusu hasira, mimi sipendagi kushindwa, hata sare sijaifurahia kwa sababu tulikuwa tunacheza nyumbani na tulikuwa tunahitaji ushindi kwa lazima,” alisema Samatta, alipozungumza na waandishi wa habari baada ya pambano hilo kumalizika.

“Haikuwa katika akili yangu kupata sare, nafikiri wachezaji wote walikuwa na hasira, sio mimi peke yangu, labda kwa sababu nilishindwa kujizuia kuionyesha, lakini hakuna mtu aliyeyafurahia matokeo,” alisisitiza Samatta.

Samatta pia alilaani staili ya ukabaji wa mabeki wa Lesotho, akisema walikuwa wanamfuata watatu kwa wakati mmoja hadi kuna wakati akajikuta anakasirika.

Kwa upande wake, Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Salum Mayanga alisema mabeki wake walifanya kosa kubwa kuruhusu goli la kusawazisha la Lesotho.

“Tumefanya makosa kuruhusu goli rahisi la Lesotho, lakini sare ya leo haitukatishi tamaa na tutaendelea na mazoezi kama kawaida kwa ajili ya mechi zilizosalia. Naamini makosa ya leo tutayafanyia kazi na tutazinduka, tutafanya vizuri,”alisema Mayanga.

Katika mechi hiyo iliyohudhuriwa na mashabiki wachache kutokana na kuchezwa usiku na pia umbali wa mahali uliko uwanja, Taifa Stars ilikuwa ya kwanza kupata bao
dakika ya 27 kupitia kwa Samatta, kwa shuti la mpira wa adhabu, baada ya beki wa kushoto, Gardiel Michael kuangushwa nje ya boksi.

Lesotho, maarufu kwa jina la Mamba, walisawazisha dakika ya 34 kupitia kwa Thapelo Tale aliyeunganisha pasi nzuri ya Jane Thaba-Ntso baada ya mabeki wa Taifa Stars kujichanganya.

No comments:

Post a Comment