KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, April 3, 2014

KOCHA AZAM ATAMBA UBINGWA NI WAO



KOCHA Mkuu wa Azam FC, Joseph Marius Omog amewataka wachezaji wake kutobweteka kwa ushindi wa jana dhidi ya Simba SC, kwani vita ya ubingwa bado ni kali na Mbeya City na Yanga SC nao pia wote wana nafasi ya kubeba taji.

Azam FC jana iliifunga Simba SC mabao 2-1 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kufikisha pointi 53 baada ya kucheza mechi 23 mbele ya Yanga SC yenye pointi 46 za mechi 22 na Mbeya City yenye pointi 45 za mechi 23.

Omog ambaye ni raia wa Cameroon amewataka wachezaji wake kuendelea kupambana kuhakikisha wanashinda mechi zote zilizosalia kama wanataka kusherehekea ubingwa. “Hakuna mechi nyepesi katika hatua hizi, hata timu inayotaka kushuka daraja inaweza kukufunga, lazima tutilie mkazo mechi zote,”alisema Omog.

Kocha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Cameroon amewapongeza wachezaji wake kwa ushindi wa jana katika mchezo mgumu na akawataka sasa kuhamishia fikra zao katika mchezo ujao dhidi ya Ruvu Shooting Aprili 6, Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

Ikitoka Mlandizi, Azam FC itakwenda Mbeya kucheza na Mbeya City Aprili 13 Uwanja wa Sokoine kabla ya kumalizia Ligi Kuu msimu huu kwa kumenyana na JKT Ruvu Aprili 19, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment