KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, December 6, 2016

AZAM YAVUNA NYOTA SITA WA U17 KIGOMA




KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, imefanikiwa kuvuna vijana sita kwenye majaribio ya wazi yaliyohusisha vijana chini ya umri wa miaka 17 (U-17), iliyoyafanya katika Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma juzi.

Huo ni mwendelezo wa programu ya mabingwa hao ya kusaka vijana nyota kutoka maeneo mbalimbali nchini, watakaounda timu ya vijana chini ya umri wa miaka 17 ya timu hiyo.

Safari hii mahudhuria yalikuwa makubwa sana kutokana na jumla ya vijana 544 kufanyiwa usaili mjini humo na benchi la ufundi la timu ya vijana ya Azam FC chini ya Mwingereza Tom Legg, anayesimamia mradi huo.

Legg anayeshirikiana kwa ukaribu na kocha mzawa kijana, John Matambara, alihitimisha zoezi hilo kwa kuchagua vijana sita bora na wengine 20 akiwaweka kwenye kumbukumbu yake kwa ajili ya kuwapa nafasi nyingine baadaye.

Takwimu zinaonyesha kuwa mpaka sasa katika mikoa yote saba ambayo imetembelewa, Dar es Salaam, Tanga, Morogoro & Dodoma, Mbeya, Mwanza, Visiwani Zanzibar na Kigoma, Azam FC imefanikiwa kuwafanyia usaili jumla ya vijana 3,809 huku waliochaguliwa wakiwa ni 89 tu na wengine 171 wakiorodheshwa kwenye kumbukumbu ya mradi huo.

Vijana wote ambao wamechaguliwa kwenye mikoa iliyotembelewa, baadaye mwezi huu wanatarajia kuitwa katika Makao Makuu ya Azam FC ‘Azam Complex’ kwa ajili ya hatua ya fainali, ambayo ndio itatoa wachezaji bora watakaounda kikosi hicho kinachotafutwa, ambacho kitaanza kupewa mafunzo kuanzia Januari mwakani.

No comments:

Post a Comment