KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, August 10, 2014

ZESCO YATIBUA SHEREHE ZA SIMBA DAY, MNYAMA APIGWA 3-0








TIMU ya soka ya Zesco ya Zambia jana ilitibua sherehe za Simba Day baada ya kuwalaza mabingwa

hao wa zamani nchini mabao 3-0 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam.

Simba ilitumia mechi hiyo kuwatambulisha wachezaji wake wapya, inayotarajia kuwasajili kwa ajili ya
msimu ujao wa ligi kuu.

Hata hivyo, maelfu ya mashabiki wa Simba waliofurika kwenye uwanja huo kuanzia saa nane mchana,
walijikuta wakigeuka mabubu baada ya kuishuhudia timu yao ikicheza soka ya kiwango cha chini na
kukubali kipigo hicho kikubwa.

Baadhi ya nyota wapya wa Simba waliocheza mechi hiyo ni pamoja na Paul Kiongera kutoka Kenya na Kwizera kutoka Burundi. Wakati Kwizera alionyesha uhai kwenye safu ya kiungo, Kiongera alishindwa kuonyesha makeke yake katika ushambuliaji.

Iliwachukua Zesco dakika 14 kuhesabu bao la kwanza lililofungwa bna Jacskon Mwanza, aliyeunganisha  wavuni kwa kichwa krosi kutoka kwa Justine Zulu, aliyemlamba chenga beki Donald Musoti wa Simba kutoka pembeni ya uwanja. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Simba ilikianza kipindi cha pili kwa kufanya mabadiliko ya wachezaji wa tano baada ya awali, Haruna
Chanongo kuchukua nafasi ya Ramadhani Singano.

Bao la pili la Zesco lilifungwa kwa njia ya penalti na Clatoos Chane dakika ya 64 baada ya kuangushwa ndani ya eneo la hatari na beki Musoti wa Simba.

Simba ilipata nafasi kadhaa nzuri za kufunga mabao katika kipindi cha kwanza, lakini zilipotezwa na
washambuliaji wake, Hamisi Tambwe, Singano na Kiongera.

Bao la tatu la Zambia lililowavunja nguvu kabisa mashabiki wa Simba lilifungwa na Mayban Mwamba
dakika za lala salama baada ya kupokea pasi kutoka kwa Ziniselemi Moyo.

Kabla ya pambano hilo, kulikuwepo na burudani mbalimbali za muziki kutoka kwa bendi ya Twanga
Pepeta International na wasanii Barnabas na Dully Sykes.

No comments:

Post a Comment