KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, March 5, 2017

SIMBA YAVUTWA MKIA


KASI ya Simba katika kuwania taji la ligi kuu ya Tanzania Bara, jana ilipunguzwa baada ya kulazimishwa kutoka sare ya mabao 2-2 na Mbeya City kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Licha ya kulazimishwa sare, Simba inaendelea kuongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 55 baada ya kucheza mechi 24, ikifuatiwa na Yanga yenye pointi 52 baada ya kucheza mechi 23.

Hata hivyo, Simba inaweza kuenguliwa kileleni iwapo Yanga itaifunga Mtibwa Sugar leo kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro. Iwapo itashinda, itakuwa mbele ya Simba kwa tofauti ya mabao ya kufunga.

Mbeya City ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 37 lililofungwa na Ditram Nchimbi, baada ya kupokea pasi kutoka kwa Raphael Daudi. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Ibrahim Ajib aliisawazishia Simba dakika ya 65 kwa mpira wa adhabu ndogo, baada ya beki Bryson Raphael kuunawa mpira nje kidogo ya eneo la hatari.

Mbeya City ilipata bao la pili dakika ya 79 kupitia kwa nahodha wake, Kenny Ally kabla ya Shiza Kichuya kuisawazishia Simba kwa njia ya penalti dakika ya 86.

No comments:

Post a Comment