KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, October 7, 2015

SAMATTA ATOA YA MOYONI



NA MWANDISHI WETU

MBWANA SAMATA, ametoboa siri kwamba kuna wakati  anashindwa kufunga mabao kutokana na aina ya mfumo wa uchezaji  wa timu ya taifa, Taifa Stars.

Samata, mshambuliaji wa kimataifa wa klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, alisema hayo juzi jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Alikuwa akijibu swali aliloulizwa kuhusu ni kwa nini amekuwa akishindwa kuifungia mabao Taifa Stars, kama anavyokuwa anapokuwa akiichezea TP Mazembe.

Samata alisema sababu nyingine inayomfanya ashindwe kucheza vizuri anapovaa jezi ya Taifa Stars, ni wachezaji wenzake kukosa uzoefu wa michuano ya kimataifa.

"Hivyo ni vyema wachezaji wazawa watoke nje ya nchi na kucheza mpira wa kulipwa kwani huko kuna mambo mengi ya kujifunza ambayo yatawafanya wawe bora zaidi wanapokuwa uwanjani," alisema Samata.

Alisema mfumo na aina ya uchezaji wa wachezaji alionao Taifa Stars ni tofauti na ule wa TP Mazembe, ambako amekuwa akishirikiana na wachezaji nyota kutoka nchi mbalimbali  za kiafrika.

"Sina maana kwamba wachezaji wa Tanzania wabaya, hapana.
Nadhani labda ni mbinu na uzoefu mdogo wa mechi za kimataifa, hilo nalo ni tatizo," alisema Samata.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, mshambuliaji huyo wa zamani wa klabu ya Simba, aliifungia TP Mazembe mabao mawili kati ya matatu, wakati timu hiyo ilipoifunga El Merreikh ya Sudan mabao 3-0 katika mechi ya nusu fainali ya klabu bingwa Afrika.

No comments:

Post a Comment