KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, November 8, 2016

SIMBA YAZIMWA, YANGA YAFUFUA MATUMAINI


BAO lililofungwa na mshambuliaji Abdalla Mguhi dakika ya 89 limeiwezesha African Lyon kuichapa Simba bao 1-0 katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Mguhi, mchezaji wa zamani wa kikosi cha pili cha Yanga, alifunga bao hilo akimalizia krosi maridhawa kutoka kwa Miraji Adam na hivyo kuamsha shangwe kwa mashabiki wachache wa African Lyon huku wale wa Simba wakiondoka uwanjani kwa majonzi.

Katika mechi nyingine ya ligi hiyo, mabingwa watetezi Yanga walifufua matumaini ya kutwaa taji hilo baada ya kuichapa Prisons bao 1-0 kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Bao pekee na la ushindi la Yanga lilifungwa kwa njia ya penalti na mshambuliaji Simon Msuva baada ya James Mwasote wa Prisons kumchezea rafu mbaya Obrey Chirwa wa Yanga.

Prisons ilipata nafasi nzuri ya kufunga bao la kuongoza dakika ya 55 baada ya kupata adhabu ya penalti, lakini shuti la Lambert Sabiyanka wa Prisons, liliokolewa na kipa Benno Kakolanya wa Yanga.

No comments:

Post a Comment