KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, November 14, 2016

NAPE AMKABIDHI BENDERA MWAKILISHI WA TANZANIA KATIKA MISS AFRICA 2016





Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Nape Nnauye,  ameahidi  kuendelea kufanya mageuzi makubwa katika mashindano ya urembo hapa nchini ili kuondoa dosari zinazojitokeza katika mashindano hayo.

Nape ametoa ahadi hiyo leo Jijini Dar es Salaam wakati akimkabidhi Bendera Mshiriki wa  Tanzania katika mashindano ya urembo Bara la Afrika kwa mwaka 2016 yatakayofanyika Novemba 28 mwaka huu nchini Nigeria.

Nnauye  ameongeza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa mashindano kama haya yanakuwa na tija kwa Taifa hasa katika kuleta ajira kwa vijana pamoja na kuitangaza nchi kimataifa kupitia urembo.

“Serikali  nia yake ni kuhakikisha kuwa jambo hili linakuwa bora, linaminiwa na kuheshimika hivyo  watanzania wote watajivunia uwepo wa mashindano ya urembo nchini” alisistiza Mhe Nnauye.

Aidha Mwakilishi wa Millen Magese group Ltd,Matukio Aranyande Chuma amesema kuwa shindano hili litailetea sifa Tanzania na ni kwa mara ya kwanza kufanyika hivyo wataitumia fursa hiyo kuitangaza nchi kimataifa kupitia urembo.

“ kwa niaba ya Millen Magese group Ltd tunatoa shukrani zetu kwa Serikali na Kamati ya Miss Tanzania kwa kutuunga mkono katika jambo hili na tunaahidi kufanya vizuri katika mashindano haya”Alisema  Chuma.

Kwa upande wake Mshiriki kutoka Tanzania anayekwenda kushiriki mashindano hayo Bi. Julietha Kabete ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuunga mkono mashindano mbalimbali ya urembo Tanzania inaposhiriki.

“Naahidi kuitangaza nchi yangu vizuri katika mashindano haya na naomba watanzania waniombee na wanipigie kura ili niweze kushinda na kuitangaza Tanzania kimataifa katika urembo” Alisema  Julietha.

Mashindano ya Miss Afrika yameanzishwa mwaka 2016 na Prof. Bena Yage ambaye ni Gavana wa Jimbo la Cross River nchini Nigeria kwa lengo kupata mabalozi wa nchi za Afrika watakaosaidia kutangaza na kuelimsha waafrika kuhusu uchumi unaozingatia utunzaji wa mazingira.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amekabidhi bendera ya Taifa kwa mlimbwende Julieth Kabete ambaye ameshiriki Shindano la Miss Tanzania na kufanikiwa kushika namba nne Julietha ambapo anakwenda nchini Nigeria kushiriki shindano ya Afrika, litakalofanyika baadae mwezi huu. Katika picha akiwa pamoja na baadhi ya waandani wa Miss Tanzania Hashim Lundenga na mwakilishi wa Milen Magese Matukio Chuma na mama mzazi wa Julieth.

No comments:

Post a Comment