KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, November 8, 2016

TWIGA STARS KUIPIMA UBAVU CAMEROON

Waandaaji wa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wanawake 2016, wameipa heshima Tanzania na kuona kuwa Twiga Stars – Timu ya Taifa ya Wanawake inafaa kuipima ubavu kabla ya kuanza kwa fainali hizo Novemba 19, mwaka huu.

Twiga Stars ambayo sehemu kubwa ya kikosi hicho kinaundwa na wachezaji wa timu ya taifa ya Wanawake ya Tanzania Bara yaani Kilimanjaro Queens ina rekodi nzuri ya kuwa kinara wa viwango vya ubora kwa nchi za Afrika Mashariki na kati lakini zaidi ni mabingwa wapya wa ukanda huo – ubingwa uliopatikana Septemba, mwaka huu huko Uganda.

Rekodi hizo zimelisukuma Shirikisho la Mpira wa Miguu la Cameroon (FECAFOOT) – nyumbani kwa Rais wa CAF, Issa Hayatou kuikubali Twiga Stars na hivyo kuomba kucheza nayo mwishoni mwa wiki ijayo. Tayari Twiga Stars imeanza maandalizi ya kutosha chini ya Makocha Sebastian Nkoma na Wasaidizi wake Edna Lema na El Uterry Mollel.

Kutokana na kuitikia wito huo kutakuwa na mabadiliko kidogo ya ratiba kwa Ligi Kuu ya Wanawake. Ligi hii itaendelea kama ilivyo kwenye ratiba kwa makundi yote mawili ya A na B, isipokuwa kwa michezo miwili tu ambayo yote ni ya Kundi A.

Mchezo kati ya JKT Queens na Viva FC kadhalika Evergreen Queens na Mlanduzi Queens, ambayo itapangiwa tarehe nyingine. Michezo yote hii ilikuwa ichezwe tarehe 09.11.2016 kwenye viwanja vya Karume na Uhuru, Dar es Salaam.

Timu za JKT Queens na Mlandizi Queens zina wachezaji zaidi ya wawili kwenye Twiga Stars ambako JKT Queens wana wachezaji 11 na Mlandizi Queens ina wachezaji watatu.

No comments:

Post a Comment