KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, December 2, 2010

Wacongo wa Yanga wakwama Dar

KLABU ya Yanga imesema, itawasajili wachezaji wake wapya, Itubu Imbem na Selenga Motitya kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wakati wa msimu wa ligi wa 2011/12.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, klabu hiyo imeshindwa kuwasajili wachezaji hao wakati wa usajili wa dirisha dogo kutokana na kushindwa kupata vibali vya uhamisho wa kimataifa kutoka klabu yao.
Wachezaji hao wawili wanatoka timu ya AFC Leopards ya Kenya, Itubu akiwa anacheza nafasi ya ushambuliaji wakati Selenga ni mchezaji wa kiungo.
Chanzo cha habari kutoka ndani ya Yanga kimeeleza kuwa, wachezaji hao wawili waliletwa nchini na Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Davis Mosha kwa ajili ya usajili wa dirisha dogo.
“Tatizo ni kwamba wachezaji hao walikuja wakati zikiwa zimebaki siku chache kabla ya usajili wa dirisha dogo kufungwa, hivyo haikuwa rahisi kufanya mazungumzo na klabu yao na kuwapatia uhamisho wa kimataifa,”kilisema chanzo hicho.
Kiliongeza kuwa, kufuatia usajili wao kukwama, uongozi umepanga kuwasajili katika ligi ya msimu wa 2011/12 iwapo benchi la ufundi litaridhishwa na viwango vyao vya soka.
Mtoa habari huyo alisema, timu hiyo inatarajiwa kuanza mazoezi kesho kwenye uwanja wa shule ya kimataifa ya Tanganyika, Dar es Salaam ikiwa chini ya Kocha Kostadin Papic.
“Lengo letu ni kuwabakisha ili tuwasajili katika ligi ya msimu ujao, lakini kabla ya kufanya hivyo, lazima tuwajaribu na kuridhishwa na viwango vyao,”alisema.
Katika usajili huo wa dirisha dogo, Yanga imefanikiwa kuwasajili mshambuliaji Davis Mwape kutoka Zambia na Juma Sefu kutoka JKT Ruvu ya mkoani Pwani.
Mwape amesajiliwa kwa ajili ya kuziba pengo la Kenneth Asamoah kutoka Ghana, ambaye klabu ya Yanga imeshindwa kupata uhamisho wake wa kimataifa kutoka katika klabu aliyokuwa akiichezea nchini Serbia.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Yanga umeshindwa kufikia makubaliano na klabu ya African Lyon kuhusu usajili wa mkopo wa kipa Ivan Knezevic kutoka Serbia.
Yanga ilipanga kumuuza kipa huyo Lyon ili ipate nafasi ya kusajili mchezaji mwingine kutoka nje ya nchi kwa vile tayari imeshafikisha wachezaji watano wanaohitajika kwa mujibu wa kanuni.
Mmoja wa viongozi wa Yanga alithibitisha jana kuwa, viongozi wa Lyon wamegoma kumnunua kipa huyo kwa mkopo kwa madai kuwa, hawamuhitaji.

No comments:

Post a Comment