KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, December 2, 2010

SAM WA UKWELI: Namshukuru Mungu, sasa nimetimiza malengo yangu


KWA kipindi cha takriban miezi mitatu sasa, kibao cha ‘Sina raha’ cha msanii Salum Mohamed Salum, maarufu kwa jina la ‘Sam wa Ukweli’, kimekuwa kikishika chati kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini.
Kushika chati kwa kibao hicho kumetokana na mambo mawili makubwa. Kwanza ni mpangilio wa ala za muziki na sauti mwanana ya mwimbaji na pili ni ujumbe uliomo kwenye kibao hicho.
Ni kibao kinachozungumzia masuala ya mapenzi, ambapo kijana Sam wa Ukweli anasikika akimlalamikia mwanadada fulani kwa kumtesa kimapenzi kiasi cha kumfanya asiwe na raha.
Akizungumza na Burudani wiki hii, Sam alikiri kuwa, kibao hicho kimempatia umaarufu mkubwa nchini kutokana na kukubalika kwa mashabiki wengi wa muziki wa kizazi kipya.
Kibao hicho ndicho kilichobeba jina la albamu yake ya kwanza yenye jumla ya vibao kumi. Mbali na ‘Sina raha’, vibao vingine vilivyomo kwenye albamu hiyo ni ‘Hata kwetu wapo’, ‘Usiniache mchumba’, ‘Lifti’, ‘Utamu ulokela’, ‘Lonely’, ‘Huwezijua’, ‘Penzi la kushare’, ‘Tunda la msimu’ na ‘Sina raha remix’.
“Kwa kweli kibao hiki kimefanya vizuri sana sokoni kuliko nilivyotarajia. Ni kibao kilichoniweka kwenye chati ya juu. Nashukuru kwamba mashabiki hivi sasa wananikubali sana,”alisema Sam.
“Nawashukuru mashabiki kwa kunisapoti. Kwa kweli hivi sasa ukitaja majina ya wasanii watatu wa muziki wa kizazi kipya hapa nchini, jina langu haliwezi kukosekana,”aliongeza msanii huyo, asiyekuwa na makeke.
Sam alisema albamu hiyo iliyoanza kuuzwa Oktoba mwaka huu na ambayo aliirekodi kwenye studio za Imotion Records za mjini Dar es Salaam, imemwezesha kutimiza mahitaji yake mengi muhimu ya kimaisha.
“Nashukuru kwamba hivi sasa napata pesa ya ugali, siwezi kufa njaa. Nina uwezo wa kununua kila ninachokihitaji kwa mahitaji muhimu ya kibinadamu,”alisema.
Sam alisema anashukuru kwamba, mafanikio ya albamu yake hiyo sokoni yametimiza malengo aliyokuwa amejiwekea baada ya safari ndefu ya kiusanii, iliyokuwa na vikwazo vya kila aina.
Alivitaja baadhi ya vikwazo alivyokuwa akikabiliana kuwa ni pamoja na kukosekana kwa studio za kurekodi nyimbo mahali alikokuwa akiishi, Kiwangwa mjini Bagamoyo mkoani Pwani.
“Kwa kweli, vikwazo nilivyowahi kukumbana navyo kimuziki ni vingi na vya kukatisha tamaa, lakini nilipiga moyo konde na kuamua kupambana navyo, nikiamini kwamba ipo siku Mungu atajibu dua zangu,”alisema.
Kufuatia mafanikio aliyoyapata, Sam alisema kwa sasa anajiandaa kurekodi wimbo mpya pamoja na video yake, akiwashirikisha wasanii chipukizi wawili, Miundombinu na Sal B kwa lengo la kuibua vipaji vyao.
Msanii huyo alisema kwa sasa, wapo wasanii wengi chipukizi wenye vipaji hapa nchini, lakini tatizo kubwa linalowakabili ni uwezo mdogo wa kifedha kwa ajili ya kurekodi nyimbo zao.
Alisema gharama za kurekodi nyimbo studio pamoja na kutengeneza kanda za video ni kubwa na kuongeza kuwa, kwa wasanii wengi chipukizi si rahisi kumudu gharama hizo.
Sam amewashukuru maprodyuza wa muziki, waandishi wa habari na watangazaji wa vituo vya radio kwa kumpa sapoti na kuzipa nafasi kazi zao kusikika na kutambulika kwa mashabiki.
Ametoa wito kwa wasanii chipukizi kufanyakazi kwa kujituma na pia kuipenda kazi yao ili iweze kuleta ushindani katika soko la muziki na kuwavutia mashabiki.
Sam, ambaye anavutiwa na wasanii Ambwene Yesaya ‘AY’ na Judith Wambura ‘Lady JayDee’, alianza kujihusisha na muziki mwaka 2005 kwa kuimba nyimbo za kuiga za wanamuziki mbalimbali wa zamani kama vile marehemu Marijani Rajabu na za bendi ya Msondo Ngoma.
Kutokana na umahiri wake wa kuiga nyimbo hizo, baadhi ya jamaa zake walimshauri ajitose kwenye fani hiyo kikamilifu kwa kutunga na kuimba nyimbo zake mwenyewe.
Hata hivyo, hakuweza kurekodi nyimbo hizo hadi mwaka 2007 baada ya kukutana na prodyuza Kisaka, ambaye alimshirikisha kwenye tamasha la kusaka vipaji lililofanyika kwenye ukumbi wa Moment Park, Kiwalani Dar es Salaam. Katika tamasha hilo, Sam aliibuka mshindi.
Baada ya kushinda tamasha hilo, Sam aliingia mkataba na Prodyuza Sam kwa ajili ya kurekodi nyimbo zake kupitia lebo ya kampuni yake na hadi sasa yupo chini ya kampuni hiyo.

No comments:

Post a Comment