KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, December 3, 2010

Wacheza filamu wanaong'ara Bongo




STEVEN KANUMBA
Amedhihirisha kwamba ujuzi wa kuigiza haupatikani kwa kukaa kwenye darasa lenye kuta nne na kujifunza, bali ni kipaji cha kuzaliwa na ubunifu wa kila mara.
Ni msanii ghali ambaye 'hakodishiki' na watayarishaji filamu wa Bongo zaidi ya wafanyabiashara wenye asili ya kiasia, maarufu kama Wadosi. Kwa sasa, Kanumba ameamua kuwa mtayarishaji filamu na pia msanii kwa wakati mmoja na ni kipenzi cha mashabiki wengi wa fani hiyo katika nchi za Afrika Mashariki. Sura yake pekee inatosha kuuza filamu husika.

VICENT KIGOSI 'RAY'
Kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, Ray ndiye msanii ghali zaidi wa kiume nchini, ambaye anapendwa na mashabiki wengi ndiyo sababu katika filamu kumi bora nchini, huwa ameshiriki katika filamu saba. Ukizungumzia filamu za Tanzania kwa sasa, unamzungumzia Ray na kipaji chake kimempa thamani kubwa mbele ya jamii.

JACOB STEVEN 'JB'
Ni msanii mwenye vituko, ambaye ukimuona akiwa mtaani kwake Sinza jijini Dar es Salaam, huwezi kuamini kuwa ndiye staa unayemuona kwenye filamu kwa jinsi anavyojirahisisha.Amekamata sehemu kubwa ya soko na asilimia kubwa ya filamu alizocheza zinafanya vizuri sokoni. Hivi karibuni, JB aliwahi kutaka ajulikane kwa jina la Amitha Bachchan, mwigizaji nyota wa zamani wa Kihindo.
SINGLE MTAMBALIKE 'RICH'
Katika wasanii waliokaa miaka mingi kwenye tasnia hiyo, Rich ni mmojawapo kwani miaka ya nyuma aliwahi kutamba katika maigizo ya televisheni. Ni msanii mwenye staili ya aina yake, ambaye muda wowote ule unatamani kumuangalia kwenye filamu na maharamia wengi wamekuwa wakinufaika kwa kuuza kinyemela kazi zake na mastaa wengine.
MZEE CHILO
Babu ndiyo jina linalomtambulisha zaidi katika fani ya filamu. Anaweza akawa ndiye msanii mwenye umri mkubwa kuliko wote kwenye tasnia ya filamu nchini, lakini hakuwahi kuwaboa mashabiki. Amefiti kwenye sehemu nyingi alizoigiza na anathibitisha usemi kuwa 'Simba hazeeki maini' kwani amekuwa akifanya vitu, ambavyo hata vijana wa kisasa hawawezi kufanya wala kuiga.
MAHSEN AWADHI 'CHENI'
Hana haja ya kutambulishwa kwa mashabiki wa filamu nchini kwani ameifanya kazi hiyo miaka mingi na uzoefu wake unamsaidia kwani anafiti kila sehemu anayoigiza.
Anazo staili zake, ambazo zimekuwa zikisisimua mashabiki wake kila wanavyomuangalia kwenye runinga na ni ngumu kutamani filamu imalizike ndiyo maana soko lake litazidi kuwa juu siku zote.
TINO
Kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, msanii huyu ni miongoni mwa mastaa wa kiume wanaopendwa sana na mabinti ndiyo maana hupenda kumtumia zaidi kwenye filamu za mapenzi.
Kila anapocheza filamu, anatoka na staili mpya na unadhifu wake pamoja na utundu imeelezwa kuwa ni miongoni mwa vitu vinavyomfanya azidi kupendwa.
CLOUD
Si msanii ghali sana kwa mujibu wa watayarishaji wa filamu, lakini cha kushangaza ni kwamba, amefanya kazi nyingi kwa kiwango cha juu, ambacho wakati mwingine huwafunika hata waigizaji maarufu zaidi yake. Yumo miongoni mwa wasanii mahiri na wenye majina makubwa nchini kuanzia kwenye maigizo mpaka filamu.
CHUZI
Ana majukumu mengi katika tasnia hiyo kwani mbali na kuwa mwigizaji, anahusika kwa kiasi kikubwa katika kutengeneza filamu na tamthilia mbalimbali, ambazo zinafanya vizuri. Amejijenga vilivyo na anadhihirisha kipaji chake kwenye runinga.
HEMED NA MLELA YUSUF
Wanachosema baadhi ya watayarishaji wa filamu ni kwamba, wasanii hawa ni wepesi wa kuelewa ndio sababu wamekuwa wakipenda kufanyanao kazi katika filamu na kung'ara, ingawa hawako miaka mingi. Wanapewa nafasi kubwa ya kuzidi kung'ara kadri siku zinavyoendelea kwa vile wamepokelewa vizuri sokoni, ingawa imewahi kuvumishwa kuwa waligombana na baadaye wakasuluhishwa.
NURDIN MOHAMMED a.ka.Chekibudi
Hadhi yake kwa mashabiki imekuwa juu sana katika miezi ya hivi karibuni kutokana na kushiriki kucheza filamu nyingi, ambazo zimefanya vizuri na sura yake imetokea sana. Imefahamika rangi yake ndiyo inachengua mashabiki wa fani hiyo hasa wa kike.
BABA HAJI NA SAJUKI
Wana miaka kadhaa kwenye fani hiyo ya uigizaji na kila kukicha wamekuwa wakifanya mambo ambayo yamekuwa yakizidi kuwakuza na kuongeza thamani yao. Ingawa wanaweza wakawa si maarufu sana kwa mashabiki kama walivyo mastaa wengine, filamu nyingi walizoigiza zimefanya vizuri sokoni.
IRENE UWOYA
Hashikiki kwa gharama. Baadhi ya watayarishaji wa filamu wamemuelezea kuwa ni msanii wa kike anayependwa zaidi kwa sasa na ghali zaidi, ingawa yeye mwenyewe amekuwa mara kadhaa akikataa.Uzuri wake, umbo na kipaji ndivyo vitu vinavyombeba. Inadaiwa kuwa ni miongoni mwa wasanii, ambao hata akiigiza upuuzi, mashabiki lazima wanunue filamu yake bila kujali.
ROSE NDAUKA
Silaha yake kubwa ni ubunifu ingawa hata uzoefu umemsaidia na kwamba yupo katika orodha ya wasanii bora watano wa kike kwa sasa kwenye filamu za Tanzania.Hakuna anayemuangalia kwenye video akaacha kutabasamu. Anaigiza kwa hisia zinazoteka akili ya mtazamaji.
AUNT EZEKIEL
Uzuri wake pamoja na staili za mavazi vinambeba, lakini neno unaloweza kutumia kumuelezea ni kwamba ana kipaji cha ukweli. Utundu wake katika kuigiza umewatoa wengi machozi kama si kuwafanya wabadili staili ya maisha kutokana na funzo wanalopata. Imeelezwa kuwa hata kashfa zinazomuandama kila siku zimemjengea jina na kumuongezea mashabiki zaidi.
JACKLINE WOLPER
Ukweli unabaki palepale kwamba ni msanii, ambaye muda wowote utavutika kumuangalia yeye binafsi au filamu aliyoigiza kutokana na staili yake na urembo aliojaliwa. Awe anaigiza kama mpenzi au mke, anafanya vizuri kazi yake kuanzia mwanzo mpaka mwisho.
MONALISA
Tofauti yake na wenzake ni kwamba ana uzoefu mkubwa, ambao pengine katika wasanii wa umri wake wanaong'ara kwa sasa, hakuna wa kumfunika kwa hilo. Wadau wanadai kuwa ni mkali kwenye uigizaji mara mbili au tatu ya Uwoya na Aunt Ezekiel, lakini wao wamekuwa maarufu zaidi kutokana na haiba zao na kashfa za kila kukicha.
JOHARI
Zilipoanza kuvuma filamu, ndio alikuwa kama malkia na wasanii wengi wa kike wanaotamba kwa sasa wamejifunza mambo mengi kutoka kwake. Ni msanii mwenye mvuto, ambaye hawezi kufanana na wenzake kutokana na ubunifu wake na kufanya mambo kwa kiwango cha juu zaidi. Wadau wanadai alistahili kuwa tajiri mkubwa kwa sasa kutokana na kipaji chake.
RIHAMA ALLY
Ni msanii mwenye kipaji cha aina yake, ambacho hakuna mtayarishaji yeyote wa filamu anaweza kupuuzia au kuacha kukitumia. Sababu kubwa ya kutumika kwenye filamu nyingi ni kutokana na kuwapa mashabiki kile wanachohitaji na anajiamini mno ndio maana hakuwahi kufanya vibaya.
MAMA KAWELE
Ukiangalia filamu yake, hutabanduka kwenye kiti kwa jinsi alivyo na uwezo mkubwa wa kucheza na hisia zake na kukusisimua kwa kile atakachokuwa akiigiza.
FLORA MVUNGI
Hazuiliki ni mjanja balaa. Kuanzia watayarishaji wa filamu mpaka wasanii wenzake wanakubaliana na hilo bila ubishi, ndiyo maana amezidi kuwa juu siku zote. Kipaji chake kinafanya filamu ionekane kamili na ndio sababu kubwa ya kupendwa.
MAYA
Yamesemwa mengi, lakini hakuna anayeweza kuwa kama yeye wala kufanya anachokifanya kwenye filamu, ndio maana wasanii wakubwa kama Ray na Kanumba wanapenda kumtumia mara nyingi kwenye kazi zao. Anateka nyoyo za watazamaji na kuwaacha kwenye ulimwengu wa kufikirika.
THEA
Wanajaribu kumpambanisha na Rihama pamoja na Aunt Ezekiel, lakini mwisho wa siku anabaki kuwa juu na kuthibitisha kwamba uzoefu ni kitu muhimu katika kila jambo. Anajua anachokifanya na mashabiki wanamfanya thamani yake izidi kupanda.
LULU
Ni binti mdogo, ambaye amejipatia umaarufu wa haraka kwa muda mfupi kutokana na kipaji alichoonyesha kwenye filamu kadhaa alizofanya chini ya Ray, lakini hata mvuto wake unachanganya wengi. Alikumbwa na kashfa za hapa na pale katika miezi ya hivi karibuni ambazo ni kubwa kushinda umri wake na zimechangia kukuza jina lake na kufanya mashabiki wamfuatilie.
MAINDA
Ray amemkubali, ingawa imekuwa ikielezwa kuwa wana uhusiano wa kimapenzi, lakini msanii huyo wa kike ni kama ametekwa kabisa na Ray kwani katika filamu zake karibu zote yumo na amefanya vizuri na thamani yake ni kubwa.
JINI KABULA
Kabula, ambaye aliwahi kuwa na uhusiano na mwanamuziki Mr. Nice, kazi zake zimemfanya amekuwa maarufu na ni ngumu kumfunika. Ni msanii mwenye kipaji cha aina yake ambaye, orodha hii ya wasanii wanaotumika sana kwenye filamu haiwezi kutimia bila jina lake kuwepo.
NORA
Ukifanya tathmini ya haraka, unaweza kusema Nora na Johari wamefunikwa na vijana wanaowika kama Uwoya na Aunt Ezekiel, lakini kwa mujibu wa maelezo ya watayarishaji wa filamu, wasanii hao ni tofauti na kila mmoja ana thamani yake na bado anakubalika sokoni.

No comments:

Post a Comment